2018-07-03 15:07:00

Maaskofu DRC wasema, tarehe 23 Desemba 2018 ni uchaguzi mkuu tu!


Baraza la Maaskofu Katoliki DRC, CENCO linasema, uamuzi wa kufanya uchaguzi mkuu nchini humo hapo tarehe 23 Desemba 2018 hauna mjadala, hadi kieleweke! Kuna haja kwa Serikali pamoja na wadau mbali mbali kuhakikisha kwamba, wanaunda mazingira yatakayopelekea uchaguzi kuwa huru, haki na amani, ili kuwawezesha wananchi wa DRC kutekeleza haki yao ya kikatiba kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato mzima wa uchaguzi unaopaswa kuleta mageuzi makubwa katika mfumo mzima wa demokrasia nchini humo!

Hii ni sehemu ya ujumbe uliotolewa hivi karibuni na Baraza la Maaskofu Katoliki DRC baada ya kuhitimisha mkutano wake wa 55 uliokuwa unafanyika huko Kinshasa. Kuna dalili za amani na utulivu, lakini katika ujumla wake, Maaskofu wanasema, hali ni tete sana nchini DRC. Hii inatokana na ukweli kwamba, kuna uvunjwaji mkubwa wa haki msingi za binadamu na kwamba, kinzani na mipasuko ya kijamii bado inaendelea kuwapekenya wananchi wa DRC. Serikali na vyama vya upinzani vinaendelea “kutunishiana misuli kwa kupimana nguvu”, lakini waathirika wakuu ni wananchi wa kawaida! Kuna makundi ya watu wenye silaha wanaohatarisha amani na usalama wa raia na mali zao. Kuna dhana ya ukabila inayoanza kujitokeza miongoni mwa wananchi wa DRC, hali inayohatarisha umoja wa kitaifa na mafungamano ya kijamii. Serikali inaonekana kutowajibika sana katika suala zima la ulinzi wa raia na mali zao.

Baraza la Maaskofu Katoliki DRC linasikitika sana kuona kwamba, baadhi ya vyama vya upinzani vinaanza kujitoa katika mchakato wa uchaguzi mkuu hali ambayo itadhohofisha nguvu ya kidemokrasia. Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki DRC kwamba, Rais Joseph Kabila atasikiliza kwa makini sauti, kili ona matamanio halali ya wananchi wake, wanaotaka kuona kwamba, Katiba ya nchi ambayo ni sheria mama inaheshimiwa na kulindwa na wote wenye dhamana hiyo. Mkataba wa Amani wa San Silvestro uliotiwa sahihi kunako tarehe 31 Desemba 2016 unapaswa kuheshimiwa na pande zote zinazohusika. Itakumbukwa kwamba, Mkataba huu ulipania kurejesha tena demokrasia na utawala wa sheria baada ya Rais Joseph Kabila kung’ang’ania madarakani hata baada ya muda wake kisheria kuwa umekwisha!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.