2018-05-11 10:24:00

Ugonjwa wa Ebola wazuka nchini Congo DRC na 17 wakisiwa kufariki!


Wizara ya afya nchini  Demokrasi ya Congo imethibitisha kuzuka upya kwa ugonjwa wa Ebola, jimboni Equateur kaskazini magharibi mwa nchi hiyo. Visa viwili vya ugonjwa huo, vimethibitishwa baada ya kufanyika kwa uchunguzi. Ujumbe wa wataalamu wa afya kutoka serikalini, shirika la afya ulimwenguni (WHO) na shirika la madaktari wasiokuwa na mipaka wamewasili kuwasili tarehe 9 Mei 2018  kwenye kijiji kilicho athirika na ugonjwa huo. Wizara ya afya imesema jibu la haraka linahitajika kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa huo ambao kwa sasa umeibuka kwenye kijiji cha Ikoko Impenge, mtaani Bikoro jimboni Equateur. 

Daktari Jean Jacques Muyembe kiongozi wa maabara ya utafiti wa ugonjwa wa Ebola na magonjwa mengine ya kuambukiza amesema kwamba kuna uwezekano mdogo wa ugonjwa huo kusambaa kwenye maeneo mengine kutokana na kwamba vijiji hivyo vinapatikana kwenye maeneo yasiyofikika kwa urahisi, ni takriban kilomita 200 msituni na mji wa Mbadaka mji mkuu wa jimbo la Equateur. Kwa sababu ugonjwa huo unadhaniwa kuibuka mwezi desemba mwaka jana lakini ni wiki iliyopita ndio wamepata taarifa.

Kwa mujibu wa taarifa ya wizara ya afya ni kwamba kuna visa 21 vya maambukizi ambapo miongoni mwake watu 17 tayari wamefariki, ndio vilisababisha kuweko na tahadhari kuhusu ugonjwa huo. Ujumbe uliopelekwa kwa ajili ya kukadiria tukio ulikuta visa vitano vya watu wenye homa na miongoni mwake watu wawili walikutwa na virusi vya Ebola. Daktari Muyembe amesema kwamba mtu wa kwanza alihofiwa kufariki kutokana na ugonjwa huo ni afisa wa polisi kwenye kijiji cha Bokatola, ambae alionekana na  dalili za ugonjwa huo . Amesema toka tarehe 3 Mei hakujaripotiwa kifo cha mtu kwenye maeneo hayo.

Hata hivyo Shirika la Afya ulimwenguni WHO limelezea kwamba liko tayari  kuunga mkono juhudi za serikali kwa  ajili ya kuutokomeza ugonjwa huo wa Ebola. WHO imesema imetenga dola milioni moja kwa ajili ya kupambana na ugonjwa wa Ebola jimboni Equateur. Ni mara ya tisa sasa toka mwaka wa 1976, Congo kutangaza mripuko wa ugonjwa wa Ebola, virusi hivyo vya aina ya zaire vinatokana hasa na ulaji wa nyama mwitu. Mara ya mwisho ugonjwa huo kuripotiwa nchini humo ilikuwa ni Mei mwaka jana kwenye jimbo la Bas-Uele ambako watu 4 walifariki miongoni mwa visa vinane vilivyothibitishwa. Hakujakueko na uhusiano wowote baina ya virusi vya Ebola Congo na vile vilivyozuka  mwaka 2014 kwenye nchi za Afrika magharibi vilivyosababisha vifo vya zaidi ya watu 11.

Sr Angela Rwezaula 
Vaticn News!

 








All the contents on this site are copyrighted ©.