2018-04-26 16:41:00

Mh. Padre Marcellin-Marie Ndabnyemb ateuliwa kuwa Askofu wa Batouri


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Sana Padre Marcellin-Marie Ndabnyemb kutoka Jimbo Katoliki la Douala, nchini Cameroon, kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Batouri. Kabla ya uteuzi huu Askofu mteule Marcellin-Marie Ndabnyemb alikuwa ni mkurugenzi mtendaji wa Chuo cha “Notre Dame des Nations di Douala”. Alizaliwa tarehe 2 Juni 1965 Jimboni Edea. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, tarehe 13 Aprili 1996 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre.

Tangu wakati huo, ameweza kutekeleza dhamana na wajibu wake wa Kipadre kama Mwalimu wa Seminari ndogo ya St. Paul di Nylon, huko Douala. Kati ya mwaka 2001 hadi mwaka 2003 alitumwa na Jimbo lake kuendelea na masomo ya juu na hatimaye, akajipatia shahada ya uzamivu katika taalimungu ya maisha ya kiroho kutoka katika “Taasisi ya Kipapa la Teresianum” iliyoko mjini Roma. Tangu mwaka 2003 hadi mwaka 2014 amekuwa ni Jaalimu na Padre wa maisha ya kiroho Seminari kuu ya Paulo VI, huko Douala. Na tangu mwaka 2014 hadi kuteuliwa kwake kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Batouri, alikuwa ni mkurugenzi mtendaji wa Chuo cha “Notre Dame des Nations di Douala”.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!

 








All the contents on this site are copyrighted ©.