2018-04-05 15:46:00

Waziri Mkuu wa Tanzania: Viwanda 3, 306 vimeanzishwa Tanzania


Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano imetekeleza kaulimbiu yake ya kujenga uchumi unaotegemea viwanda na kwamba, hadi kufikia Februari 2018, viwanda vipya 3,306 vimekwishaanzishwa nchini. Ametoa kauli hiyo Jumatano, Aprili 4, 2018 Bungeni mjini Dodoma, wakati akiwasilisha taarifa ya mapitio ya utekelezaji wa kazi za Serikali kwa mwaka 2017/2018 na mwelekeo wa kazi za Serikali kwa mwaka 2018/2019 kwenye mkutano wa 11 wa Bunge. Amesema Serikali inahamasisha uwekezaji katika viwanda kwa kutoa vivutio vya kodi na visivyo vya kodi kwa wawekezaji mahiri (strategic investors); kuendeleza na kuboresha miundombimu wezeshi kama vile barabara, reli, bandari, umeme na maji. “Serikali itaendelea kuhuisha sera, sheria na kanuni pamoja na kufuatilia utendaji wa viwanda vilivyobinafsishwa na kuchukua hatua stahiki kwa wamiliki walioenda kinyume na mikataba ya mauzo,” amesema.

Waziri Mkuu amelieleza Bunge kwamba mikoa na Halmashauri zote nchini zimeelekezwa kutenga maeneo ya uwekezaji kwa ajili ya viwanda na kwamba katika mwaka 2018/2019, Serikali itatoa kipaumbele katika kutekeleza miradi ya kielelezo, uanzishwaji wa kanda maalum za kiuchumi pamoja na kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji katika sekta ya viwanda. Akitoa ufafanuzi kuhusu ushiriki wa sekta ya hifadhi ya jamii kwenye ujenzi wa uchumi wa viwanda, Waziri Mkuu amesema pamoja na miradi mingine NSSF na PPF kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza wanatekeleza mradi mkubwa wa uzalishaji wa sukari mkoani Morogoro.

“Lengo la mradi huo ni kuzalisha tani 250,000 za sukari na umeme megawati 40. Mradi huo unatekelezwa katika shamba la Mkulazi lililopo Ngerengere lenye ukubwa wa hekta 63,000 na shamba la gereza la Mbigiri lenye ukubwa wa ekari 12,000 lililopo Dakawa,” alisema. “Hadi sasa ekari 2,000 za mashamba ya miwa zimetayarishwa katika eneo la Mkulazi na ekari 1,100 zimepandwa miwa. Lengo la Serikali ni kukamilisha awamu ya kwanza ya ufungaji wa mitambo ya kiwanda cha Mbigiri ifikapo mwezi Desemba, 2018 ili uzalishaji uanze mwaka 2019,” alisema na kuongeza kuwa miradi hiyo itakapokamilika, itazalisha zaidi ya ajira 100,000.

Waziri Mkuu alisema tangu kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo Juni 2017, ajira za moja kwa moja 780 na ajira zisizo za moja kwa moja  24,000 ikijumuisha wakulima wadogo wa mbegu na kilimo cha nje zimezalishwa. Akifafanua kuhusu ujenzi wa barabara kuu, Waziri Mkuu alisema Serikali inaendelea kuboresha mtandao wa barabara nchini ambapo katika kipindi cha Julai 2017 hadi Februari 2018, ujenzi wa Km. 776.45 za barabara kuu kwa kiwango cha lami umekamilika na Km. 1,760 zinaendelea kujengwa. Pia barabara zenye urefu wa Km. 17,054 zilikarabatiwa katika kipindi hicho.

Kuhusu ujenzi wa madaraja, Waziri Mkuu alisema madaraja ya Kilombero na Kavuu ujenzi wake umekamilika na kwamba ujenzi unaoendelea hivi sasa ni wa madaraja ya Sibiti, Mto Mara, Lukuledi, Ruhuhu, Momba na Mlalakuwa. Alisema madaraja mengine 996 katika maeneo mbalimbali nchini yamekarabatiwa. Kuhusu jitihada za Serikali kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, Waziri Mkuu alisema hadi kufikia Februari 2018, ujenzi wa barabara ya juu katika eneo la TAZARA ulikuwa umefikia asilimia 70 na ujenzi wa barabara za juu katika makutano ya Ubungo (Ubungo Interchange) umeanza. “Maandalizi ya awamu ya pili hadi ya nne ya mradi wa ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka yanaendelea. Katika mwaka 2018/2019, Serikali imepanga kujenga kilometa 597 za barabara kuu na za mikoa kwa kiwango cha lami na kilometa 72 za kiwango cha lami zitakarabatiwa,” alisema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuliarifu Bunge juu ya uanzishwaji wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tanzania Rural and Urban Roads Agency – TARURA) kwa lengo la kurahisisha huduma za usafirishaji na kuongeza kasi ya wananchi kujiletea maendeleo. Alisema TARURA imepewa jukumu la kusimamia ujenzi na matengenezo ya mtandao wa barabara zenye urefu wa kilometa 108,946.2 za vijijini na mijini. “Katika mwaka 2017/2018, TARURA imesimamia matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 4,183.3, madaraja 35, makalavati makubwa 43 na madogo 364 na drift nne,” alisema.

Waziri Mkuu ameliomba Bunge likubali kupitisha sh. 143,618,762,698 zikiwa ni makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizopo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2018/2019 ambapo sh. 74,527,321,698 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. 69,091,441,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Vilevile, Waziri Mkuu aliliomba Bunge liidhinishe sh. 125,521,100,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge ambapo sh. 117,205,487,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na sh. 8,315,613,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

S. L. P. 980,

41193 - DODOMA.

JUMATANO, APRILI 4, 2018

 








All the contents on this site are copyrighted ©.