2018-03-22 14:32:00

Maaskofu Katoliki Urusi watuma salam za pongezi kwa Rais Putin


Baraza la Maaskofu Katoliki Urusi limetuma salam za pongezi kwa Rais Vladimir Putin kwa kuchaguliwa tena kuiongoza Urusi inayowajumuisha watu kutoka mataifa na dini mbali mbali ambao wamewekeza imani na matumaini yao kwa Rais Putin. Dhamana kubwa mbele yake kwa sasa inapaswa kujielekeza zaidi katika ustawi, maendeleo na mafao ya wengi. Baada ya mchakato wa uchaguzi mkuu ambao kwa kawaida unaacha madonda na machungu kati ya watu, kuna haja kwa sasa kuendelea kujizatiti kujenga misingi ya: haki jamii, amani na utulivu sanjari na maendeleo endelevu!

Askofu Clement Pickel, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Urusi katika ujumbe wake wa matashi mema kwa Rais Putin, anasema, Kanisa liko bega kwa bega pamoja naye, ili kumsindikiza kwa sala, ili hatimaye, aweze kutekeleza matamanio halali ya wapiga kura wake sanjari na kukuza uhusiano mwema kati ya Serikali na Kanisa. Baraza la Maaskofu Katoliki Urusi linapenda kumhakikishia Rais Putin kwamba, Kanisa liko tayari kuchangia ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kukuza na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kimaadili na kiutu sanjari na kudumisha amani na utulivu katika mazingira ya Urusi. Ni matumaini ya Mama Kanisa kwamba, kwapamoja watashikamana kupambana na baa la umaskini katika jamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.