2018-03-12 10:32:00

Askofu mkuu Nwachukwu ateuliwa kuwa Balozi wa Vatican huko Suriname


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Fortunatus Nwachukwu kuwa Balozi mpya wa Vatican kwenye Jamhuri ya Suriname iliyoko Kaskazini Mashariki mwa Bahari ya Atlantic, Amerika ya Kusini. Ataendelea pia kuwa ni Balozi wa Vatican kwenye Visiwa vya Saint Lucy, Grenada na Bahamas. Ataendelea kuwa ni Balozi wa Vatican huko Trinidad na Tobago, Antigua na Barbuda, Barbados, Dominica, Jamaica, Saint Kitts na Nevis, Saint Vincent na  Grenadines, Guyana, na pia ni Mjumbe wa kitume wa Visiwa vya Antilles.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alimteua Monsinyo Fortunatus Nwachukwu kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Nicaragua pamoja na kumpandisha hadhi ya kuwa ni Askofu mkuu hapo tarehe 12 Novemba 2012. Akawekwa wakfu kuwa Askofu mkuu tarehe 6 Januari 2013. Kabla ya uteuzi wake, alikuwa ni Afisa Mwandamizi wa Itifaki mjini Vatican. Askofu mkuu Fortunatus Nwachukwu alizaliwa Ntigha, Nigeria kunako tarehe 10 Mei 1960. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 17 Juni 1984. Monsinyo Fortunatus Nwachukwu Alianza kutoa huduma za kitume mjini Vatican tarehe Mosi, Julai 1994. Amewahi kufanya kazi katika Balozi za Vatican nchini Ghana, Paraguay, Aligeria na kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zenye makao yake mjini Geneva.  Kunako tarehe 4 Septemba 2007, aliteuliwa kuwa ni Afisa Mwandamizi wa Protakali mjini Vatican.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.