2018-02-08 15:09:00

Papa Mstaafu Benedikto XVI asema, afya inaendelea kudhohofu na uzee!


Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI tangu alipong’atuka kutoka madarakani kunako mwaka 2013, alisema wazi kwamba, anakwenda “kujichimbia kwenye Monasteri ya “Mater Ecclesiae” kwa ajili ya kutafakari, kusali na kuliombea Kanisa la Kristo ili liweze kusonga mbele. Mara chache sana, Papa Mstaafu Benedikto XVI amekuwa na mikutano na shughuli za hadhara tangu wakati huo. Takribani miaka mitano imekwisha yoyoma, tangu tukio hili lilipoutikisa ulimwengu kwani kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 600 ya maisha na utume wa Kanisa, Khalifa wa wa Mtakatifu Petro alikuwa anang’atuka kutoka madarakani kutokana na kuendelea kudhohofu kwa afya yake iliyoambatana na umri mkubwa!

Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI, hivi karibuni amemwandikia ujumbe mfupi Bwana Massimo Franco, Mwandishi wa Habari wa Gazeti la “Il Corrierre della Sera” na kuchapishwa kwenye gazeti hilo Jumatano tarehe 7 Februari 2018, akijibu dukuduku za wasomaji wa gazeti hili waliotaka kufahamu hali yake ya afya! Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI anasema, anamshukuru Mwenyezi Mungu anayemjalia maisha, kwani kutokana na uzee, afya yake inaendelea kudhohofu siku kwa siku na kwamba, kwa sasa anajiandaa kwa hija ya kuelekea nyumbani kwa Baba wa milele, kwa ajili ya usingizi wa amani. Papa Mstaafu Benedikto XVI anamshukuru Mungu kwa kumjalia zawadi kubwa ya kuweza kuzungukwa na umati mkubwa wa watu wanaomwonjesha huruma na upendo katika safari hii ambayo wakati mwingine inachosha. Huu ni upendo ambao kamwe hakuwahi kuufirikia hata kidogo katika maisha yake!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.