2018-01-27 10:15:00

Jamhuri ya Haiti na Vatican zaonesha nia ya kushirikiana zaidi


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 26 Januari 2018 amekutana na kuzungumza na Rais Jovenel Moïse wa Jamhuri ya Haiti, ambaye, baadaye amekutana pia na kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican. Katika mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na mgeni wake Rais Jovenel Moïse, wameridhishwa na uhusiano wa kidiplomasia ulipo kati ya Vatican na Haiti na kwamba, wameonesha nia ya kutaka kuimarisha uhusiano huu ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali za kijamii, lakini hasa zinazowakumba vijana wa kizazi kipya, maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Viongozi hawa wameridhishwa pia na mchango wa Kanisa katika ustawi, maendeleo na mafao ya wananchi wa Haiti hasa katika sekta ya elimu, huduma ya afya na ushuhuda wa Injili ya upendo! Katika mwendelezo wa mazungumzo yao, Baba Mtakatifu pamoja na mgeni wake, wamekazia masuala ya kitaifa na kikanda, hususan tatizo na changamoto kubwa ya wakimbizi na wahamiaji; umuhimu wa kukuza na kudumisha majadiliano katika ukweli na uwazi, ili kuimarisha mafungamano ya kijamii pamoja na ustawi, mafao na maendeleo ya wengi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.