2018-01-25 10:56:00

Kard. Laurent Monsengwo akemea ukatili na uvunjwaji wa haki msingi


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Katekesi yake siku ya Jumatano, tarehe 24 Januari 2018 ametumia nafasi hii kuwalika wananchi wote wa DRC kujizatiti katika mchakato wa ujenzi wa msingi wa haki, amani na maridhiano: kwa kuondokana na ghasia na mipasuko ya kijamii. Kanisa nchini DRC kwa upande wake, litaendelea kujizatiti katika mchakato wa ujenzi wa amani, ustawi na maendeleo ya wengi nchini humo! Hii ni changamoto pevu na endelevu!

Kardinali Laurent Monsengwo Pasinya, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Kinshasa, DRC anasema, Kanisa litaendelea kusimama kidete kupinga vitendo vyote vinavyovunja haki msingi za binadamu na kudhalilisha utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Anasema, Serikali ya Rais Joseph Kabila, Jumapili iliyopita, tarehe 21 Januari 2018 imetumia nguvu kubwa ya kijeshi dhidi ya raia waliokuwa wana andamana kwa amani. Kwa sasa Kinshasa inaonekana kuwa kama ni gereza wazi. Kuna watu wanaendelea kupoteza maisha, kupata majeraha na kutupwa kizuizini, bila kuzingatia haki msingi za binadamu. Inawezekanaje, vyombo vya ulinzi na usalama, vikawafyatulia risasi watu wanaosali Rozari, wanaoimba nyimbo na tenzi za maombolezo; watu wanaokumbatia Msalaba kudai haki zao msingi? Anahoji, Kardinali Laurent Monsengwo Pasinya.

Matumizi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji huko Jamhuri ya Watu wa Congo yameshtumiwa pia na Umoja wa Ulaya. Ni matukio ambayo yanakwenda kinyume kabisa cha dhamana na wajibu wa Serikali ya Rais Joseph Kabila ya kuandaa hali na mazingira yatakyosaidia kuanzisha tena mchakato wa uchaguzi mkuu, ili kweli demokrasia iweze kurejea tena nchini DRC. Umoja wa Ulaya unaitaka Serikali kufanya uchunguzi wa kina, ili wahusika wa vitendo vya uvunjifu wa haki msingi za binadamu na nyanyaso dhidi ya raia wanafikishwa mbele ya Sheria, ili iweze kuchukua mkondo wake. Ni matumaini ya viongozi wa Kanisa kwamba,  Padre Roberto Masinda bado yuko hai na ataweza kuachiliwa huru wakati wowote! Habari zaidi kutoka DRC, Alhamisi, tarehe 25 Januari 2018 zinasema, Padre Roberto Masinda ameachiliwa huru. Huyu alikuwa ni Padre wa sita kutekwa nyara Jimbo Katoliki Butembo, DRC tangu mwaka 2012 hadi leo hii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.