2018-01-04 14:05:00

Papa Francisko asikitishwa na ajali ya barabarani iliyofyeka watu 48


Baba Mtakatifu Francisko ametuma salam za rambi rambi Jimbo kuu la Lima kufuatia ajali mbaya ya Bus iliyotokea Jumanne, tarehe 2 Januari 2018 huko Serpentin de Pasamayo nchini PerĂ¹ baada ya Trekta kugongana na Bus la abiria lililokuwa na abiria 50 na kusababisha abiria 48 kupoteza maisha! Baba Mtakatifu katika salam za rambi rambi zilizoandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema, anapenda kuonesha uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala na sadaka yake kwa wale wote waliofikwa na msiba huu. Baba Mtakatifu anawaombea marehemu pumziko la amani na wale waliopata majeraha kupona haraka ili hatimaye, waweze kuendelea tena na shughuli zao!

Taarifa zinaonesha kwamba, Bus lilitumbukia katika korongo kubwa lililoko kwenye eneo la Bahari ya Pacific. Idadi ya watu waliofariki inaweza kuongezeka mara dufu. Baba Mtakatifu anawatakia wote amani, utulivu na matumaini ya Kikristo katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo. Kwa wale wote walioguswa na msiba huu, anapenda kuwapatia baraka yake ya kitume!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.