2017-12-02 11:15:00

Papa amewambia Mapadre na Watawa kuchambua mbegu njema dhidi ya mbaya!


Ni dakika za mwisho wa ziara ya 21 ya kitume ya Baba Mtakatifu Barani Asia: Baba Mtakatifu atawasiri mjini Roma kwa ndege saa tano za usiku masaa ya Ulaya. Siku yake ya tarehe 2 Desemba 2017, imefunguliwa na Misa ya faragha katika Ubalozi huko Bangladesh na baadaye ameacha Ubalozi wa Kitume na kuondoka kwa gari kuelekea katika nyumba ya Mama Teresa wa Kalkuta, katika mtaa wa Tejgaon katika Parokia ya Rosari Takatifu. Ni Paroki ya Kanisa la kizamani iliyojengwa na Wamisionari wa Ureno ambapo ndani ya Parokia hiyo yapo makaburi ya wakristo.

Tejgaon ni moyo wa kimisionari nchini Bangladesh mahali ambapo mwaka 1580, walifika mapadre wa kwanza wa kireno wa Shirika la Mtakatifu Agostino na kupewa ruhusa na mfalme wa wakati huko kujenga Kanisa, masoko na maduka. Kwa njia hiyo, Baba Mtakatifu amebariki makaburi hayo mahali ambapo wamelala wamisionari  na wakristo wengine, baadaye ameelekea katika Nyumba ya Mama Teresa wa Kalkuta kuwakumbatia na kuwasalimia watu wanaoshi humo, yatima na wagonjwa.  Wakati huo huo katika Kanisa  la Rosari Takatifu alikuwa anasubiriwa na umati karibia watu 1500, wakiwa ni watawa, mapadre , waseminari na manovizi ambao ametoa ushauri wake, hasa jinsi ya kuweza kuishi maisha yao mema ya kijumuiya.

Baba Mtakatifu Francisko akitoa ushauri huo bila kusoma maandishi amesema,wito ni mbegu ya kufanya ikue na kuitunza kwa ukarimu na makini dhidi ya shetani ambaye mara kwa mara anapanda magugu mabaya, pia ni lazima kujifunza kutenganisha mbegu iliyo njema na ile mbaya. Kutokana na umakini huo, amesema, jumuiya zao: kiasikofu, mapadre, watawa wa kike na kiume, waseminari, ni lazima wawe makini, kutokana na migawanyiko inayosababishwa na masengenyo au na maneno. Baba anafafanua kuwa, masengenyo na maneno ni adui wa umoja. Anatoa ushauri kwamba, iwapo kuna jambo juu ya ndugu mwingine, ni bora kumwambia uso kwa uso, kuliko kumzunguka nyuma.

Aidha amewaonya kama watawa, kwamba, kamwe wasionesha uso wa huzuni, hata mbele ya matatizo, bali, kila mara watafute amani na watapata furaha katika maisha yao na kushuhudia. Hotuba ya Baba Mtakatifu iliyokuwa  imeandaliwa rasmi kwa ajili yao, imekabidhiwa kwa maaskofu ili iweze kusomwa katika jumuiya zao mahalia.

Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican

 

 

 








All the contents on this site are copyrighted ©.