2017-11-18 15:52:00

Zimbabwe:Muungano wa Makanisa yalilia utulivu na amani Zimbabwe!


Baada ya Rais Robert Mugaba kuwekwa chini ya ulinzi na  jeshi la nchi yake siku ya Jumatano, hatua inayochukuliwa kama ni  mapinduzi ya kijeshi, Viongozi wa Kanisa Zimbabwe, Umoja wa Afrika (AU) na wadau wengine, mbalimbali wametoa kauli zao juu ya hilo, wengi wakiomba kudumishwa kwa utulivu na amani chini Zimbabwe.    

Viongozi wa Umoja wa Kiekumeni Zimbabwe,  likiwemo Baraza la Maaskofu Katoliki, wametoa tamko lao, liiliochapishwa siku ya Jumatano na Shirika la habari la Sir, ambamo wameonyesha kujali hofu na wasiwasi uliogubika  raia wengi wa Zimbabwe , na mabadiliko yaliyofanyika , na kwamba siku hadi siku hali ya usalama inazidi kudidimia.

Viongozi wa Kanisa wanasema, wanaiona hali halisi ya kisiasa, si tu kama kipeo, lakini pia kama mwanya wa kuunda taifa jipya la Zimbabwe. Viongozi wanatolea maombi yao kwa Mwenyezi Mungu, mwenye kujua matatizo yote ya taifa lao, awaongoze katika kupata jibu linalofaa kutembea pamoja  kama taifa. Na wametaja matatizo makubwa yanayokabili Zimbabwe kwamba ni watu kukosa  imani na taasisi za kisheria na taasisi za umma, ikiwemo  ukosefu wa uwazi katika kutenganisha madaraka kati ya Chama Kikuu na serikali,  na kusahaulika kwa huduma inayoweza kuikwamua jamii iliyosahaulika katika dimbwi la umaskini.

Aidha Viongozi wa kanisa wanaona utendaji mtu kidemokrasia, unakwamishwa na ukiritiba binafsi kisiasa, hivyo kufanya maamuzi ya raia kuwa hayana tena umuhimu katika utendaji wa kisiasa.   Nalo Kanisa kwa upande wake limepoteza msukumo wake wa kinabiii, likishinikizwa na   utamaduni wa ubinafsi na ushirikina, katika  kupambana na changamoto za kijamii na kisiasa. Kwa mtazamo huo , Kanisa linatoa mwaliko kwa raia wote, kufanya mapinduzi kiroho, kwa sala, tafakari na toba,  kama ilivyoelezwa katika barua ya kichungaji ya Maaskofu juu ya hali halisi za Zimbabwe.
Viongozi wa Kanisa pia wameomba uwepo wa majadiliano kwa ajili ya kukabiliana na hali halisi kwa kuwa hakuna njia nyingine ya kupata ufumbuzi katika matatizo yao, isipokuwa kwa majadiliano ya pamoja. Wameasa bila moyo wa mapatano na tafakari za pamoja juu ya hali ya baadaye ya Zimbabwe, hakuna njema litakalofanyika Zimbabwe.

Robert Mugabe mwenye umri wa miaka 93, ambaye ameishika madaraka ya Rais tangu Zimbabwe ilipojipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza mwaka 1980 , ameingia katika msukosuko huo, baada ya uwepo wa mvutano wa nani atamrithi, hasa baada ya Makamu wa rais, Emmerson Mnangagwa kufutwa kazi na Mugabe  wiki iliyopita, kama fursa kwa  mke wa Mugabe, Grace kuwa kumrithi wa Mugabe. Hatua hiyo ilisababisha maafisa wa vyeo vya juu jeshini kwa na hisia za  kutengwa na hivyo kumzuia Rais Mugabe nyumbani kwake.

Ingawa hakuna taarifa rasmi, inasemekana baada mazungumzo na ujumbe kutoka Kanda hiyo,  Rais Mugabe, amekataa  kung’atuka madaraka mara moja licha ya kuongezeka wito wa kumtaka ajiuzulu. Naye Kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai alisema mapema kuwa,  kwa manufaa ya raia wa Zimbabwe, Mugabe anastahili kujiuzulu mara moja.

Janeth T. Mhella
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican

 








All the contents on this site are copyrighted ©.