2017-08-23 10:58:00

Askofu Mkuu Kinyaiya atoa Kipaimara kwa waamini 88 Jimbo kuu Dodoma


Bikira Maria amekuwa ni hujaji wa kwanza katika historia nzima ya ukombozi wa mwanadamu, pale alipokubali kwa moyo radhi kabisa kushiriki katika mpango wa Mungu, kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu, kiasi cha kujiaminisha mbele ya mwenyezi Mungu na kupokea kwa wasi wasi na furaha kubwa moyoni mwake ujumbe kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu yaani “Theotokos”. Akajulishwa ujumbe wa furaha kwamba, binamu yake Elizabeti, amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake, yeye aliyeitwa tasa! Kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana mbele ya Mwenyezi Mungu.

Bikira Maria akaondoka kwa haraka kwenda kumhudumia binamu yake, kielelezo makini cha mtume wa Yesu, aliyejisadaka bila ya kujibakiza, kiasi hata cha kudiriki kusimama chini ya Msalaba na kupokea maiti ya mwanaye mpendwa, Kristo Yesu! Bikira Maria ni mfano na kielelezo cha imani, matumaini na mapendo ambaye amediriki kuwa ni mfuasi wa Mwanaye mpendwa Yesu Kristo na jirani zake kwa njia ya huduma. Bikira Maria ni mfano wa imani, huduma na matumaini kwa familia ya Mungu, mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa kweli ni vyombo na mashuhuda wa huruma na upendo wa Mungu kwa jirani zao.

Mapokeo ya tangu mwanzoni mwa Karne ya V yanaonesha Ibada kwa Bikira Maria, aliyeonekana katika utukufu kwa kupalizwa mbinguni, lakini zaidi ile Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu, iliyojidhihirisha kwa namna ya pekee wakati wa maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Efeso, kunako mwaka 431, ulipotamka kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Mungu, kuwa ni sehemu ya Mafundisho Tanzu ya Kanisa. Waamini wa Kanisa la Mashariki kwa miaka mingi walikuwa wanaadhimisha Siku kuu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni kwa kielelezo cha kulala usingizi "Dormitio".

Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI aliwahi kusema kwamba, Fumbo la Bikira Maria kupalizwa mbinguni linakwenda sanjari na Fumbo la Pasaka, kiini cha ukombozi wa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Ni ukombozi uliopatikana kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu. Bikira Maria ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, hivyo, anashirikishwa kwa namna ya pekee, katika Fumbo la Pasaka na utukufu wa Kristo. Ni Fumbo linaloonesha historia ya ubinadamu na matumaini ya waamini na Kanisa zima. Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni mwili na roho anaendelea kuliombea Kanisa ambalo bado liko safarini, ili liweze kupata neema ya uzima wa milele; Bikira Maria anawalinda watoto wa Kanisa ambao bado wako safarini bondeni huku kwenye machozi, ili waweze kufika salama mbinguni.

Katika mazingira ya furaha ya kusherehekea Siku kuu ya Bikira Maria Mbinguni, tarehe 13 Agosti 2017 sanjari na kilele cha maadhimisho ya Mwaka wa Padre Tanzania, yaliyofanyika Jimbo kuu la Dodoma, Askofu mkuu Beatus Kinyaiya wa Jimbo Katoliki la Dodoma aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya Bikira Maria Mama wa Damu Azizi ya Yesu inayoendeshwa na Wamissionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu nchini Tanzania. Katika maadhimisho haya, Askofu mkuu Kinyaiya ametoa Sakramenti ya Kipaimara kwa waamini 88 pamoja na kubariki nyumba ya Mapadre ambayo imejengwa na waamini kwa ajili ya kusogeza huduma ya maisha ya kiroho Parokiani hapo.

Wamisionari hawa walikuwa na upeo mpana kwa kusoma alama za nyakati na kutambua mahitaji makubwa ya maisha ya kiroho kutokana na kupanuka kwa mji wa Dodoma. Kwa sasa Parokia inahudumiwa na Padre Perfect Leiya kama Paroko akisaidiana na Padre Innocent Miku, kama Paroko usu! Askofu mkuu Beatus Kinyaiya amewataka wanaparokia hawa kusimama kidete katika misingi ya imani, matumaini na mapendo na kamwe wasikubali kuyumbishwa na mawimbi makubwa ya bahari, bali wasimame imara katika imani na kutambua kwamba, Kristo Yesu yupo pamoja nao hadi utimilifu wa dahali. Kristo yuko tayari kuwashika mkono na kuwainua kama alivyofanya kwa Petro mtume, alipoanza kuzama baharini alipoingiwa na kiguguzimi cha imani kwa kujitafuta mwenyewe.

Askofu mkuu Beatus Kinyaiya amewataka waamini kuhakikisha kwamba, wanakuwa imara na thabiti katika imani ambayo ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kuwa tayari kuishuhudia katika matendo ya huruma:kiroho na kimwili, kielelezo thabiti cha imani tendaji, yenye mvuto na mashiko kwa maisha ya watu! Wakristo wajitahidi kuwa kweli ni vyombo na mashuhuda wa huruma ya Mungu kwa waja wake, ili watu wengine waweze kuyaona na hatimaye, kuyaiga matendo yao, tayari kumtukuza Mwenyezi Mungu na kumfuasa Kristo Mkombozi wa ulimwengu.

Waamini walioimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara, wamepigwa chapa ya mhuri wa Roho Mtakatifu anayewaimarisha kuwa kweli ni askari wa Kristo Yesu, tayari kusimama kidete kuilinda na kuineza imani yao kwa njia ya matendo yenye mvuto na mashiko kwa watu wanaowazunguka. Kwa njia ya Kipaimara, wameimarishwa na sasa wanapaswa kuwajibika barabara katika maisha na utume wa Kanisa. Waendelee kuboresha maisha yao kwa njia ya sala na ibada; kwa tafakari ya Neno la Mungu na matendo ya huruma. Wajitahidi kujiunga na vyama vya kitume, vitakavyowasaidia kuimarisha imani na maisha yao ya Kikristo!

Parokia ya Bikira Maria Mama wa damu Azizi ya Yesu inaundwa na vigango vinne navyo ni: Mtakatifu Paulo wa Msalaba na Maweni vilivyoko eneo la Nzughuni; Mtakatifu Maria De Mathias pamoja na Mtakatifu Anna; ambavyo kwa pamoja viko katika mchakato wa ujenzi wa Kanisa litakalokidhi mahitaji ya watu wa familia ya Mungu Parokiani hapo. Ramani na michoro ya Kanisa tayari imekwisha kupitishwa na linakadiriwa kwamba, hadi kumalizika kwake, litagharimu kiasi cha shilingi bilioni moja za kitanzania.

RISALA YA PAROKIA-KISASA DODOMA – 2017 KWA BABA ASKOFU MKUU BEATUS KINYAIYA WA JIMBO KUU KATOLIKI DODOMA 13/08/2017 KWENYE ZIARA YA KICHUNGAJI PAROKIANI KISASA

A: Historia ya Parokia

Parokia hii ilianzishwa rasmi tarehe 02/01/2011 kutoka Parokia ya Makole na kukabidhiwa kwa Wamisionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu kama sehemu ya Utume wao katika Jimbo Kuu Katoliki Dodoma. Inaitwa : – KISASA kutokana na nyumba za serikali takribani 300 zilizojengwa katika eneo hilo zikiwemo pia barabara, maji na umeme. Miradi hii ya maendeleo ilifanya eneo hili kuitwa eneo la Kisasa. Somo wa Parokia yetu ni Bikira Maria Mama wa Damu Azizi ya Yesu. Idadi ya Familia katika Parokia: ni 1,223. Idadi ya waamini Wakatoliki kwa kadiri ya Sensa iliyopita ni 4892.  Idadi ya Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo ni 52. Tuna Jumla ya Vigango Vinne:

Mt Anna-Medelii yalipo makao ya Parokia yetu ya Kisasa

Mt Maria de Mathias Nyumba 300

Mt. Paulo wa Msalaba Nzuguni Maweni

Mt. Yohane Mbatizaji Nzuguni Sokoine

Parokia hii inahudumiwa na Mapadre wawili: Padre Perfect Leiya-Paroko na Padre Innocent Miku-Paroko Msaidizi. Kutokana na Ukubwa wa Parokia tumekuwa tukishirikiana kwa karibu sana na Wamisionari wetu wanaofanya utume Makao Makuu ya Kanda ya shirika letu pamoja na wale wanaofanya kazi St. Gaspar Hotel and Conference Centre. Tunao jumla Makatekista sita ambao wanatusaidia katika kuwandaa waamini wenzetu kupata sakramenti mbali mbali. Pia mwaka huu tumepeleka vijana wawili kwenye chuo cha Makatekista Kibakwe hapa Dodoma ambao wataongeza nguvu katika ufundishaji dini mashuleni. Tunapenda kumshukuru Mama Mwenda ambaye ni Mwalimu mstaafu aliye kubali kusaidia kufundisha dini mashuleni. Tunamwomba Mungu ampe afya njema na baraka tele.

Tukitambua kuwa mashirika ndiyo yanayoleta uhai katika Parokia, tunafanya juhudi kadiri inavyowezekana kuwahimiza waamini wetu kwa semina mbali mbali ili waweze kujiunga na mashirika hayo.Mpaka sasa tuna Mashirika ya Kitume 8 yaliyo hai,nayo ni:  Kwaya ya Shirikisho Parokia; Aloyce Gonzaga(Watumishi), Moyo Mtakatifu wa Yesu, UWADO, WAWATA, VIWAWA,  VIPAPA, Wakarismatik Katoliki.

Lengo letu kama Parokia ni kueneza upendo wa Kristo na kukuza Umoja wa Watoto wa Mungu, kujituma kwa kufanya juhudi za dhati zenye lengo la kulea,kulinda na kuimarisha imani. Kujitahidi kulea dhamiri na kujenga maadili bora miongoni mwa waamini wa rika zote, kushikamana na kujituma katika juhudi za kuijenga Parokia na kulitegemeza Kanisa na utume wake Mtakatifu. Kushirikiana na Wanashirika wenzetu katika Nyumba ya Kisasa na Kanda ya Dodoma na wadau wote wa Uinjilishaji wakiwemo wenye Daraja, Watawa na Walei. Pia kukuza Ushirikiano na ngazi nyingine za Kanisa kama vile Dekania ya Mt. Paulo wa Msalaba, Kanda ya C.PP.S Tanzania, Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, Madhehebu na Dini Nyingine, Kanisa zima la Tanzania na Ulimwengu. Kukuza na kudumisha sauti ya unabii na Ushuhuda wa Maisha unaotupasa kama Wamisionari wa Damu Takatifu ya Yesu hapa Tanzania na Ulimwengu mzima.

Ili tuweze kufanikisha haya yote zipo shughuli mbali mbali za kichungaji na kimaendeleo zinazofanyika katika Parokia yetu. Shughuli ambazo zimefanyika mwaka huu tangu January mpaka Augost  ni kama ifuatavyo: Misa za Jumapili kwa Vigango vyote na Misa kila siku saa 12:30 asubuhi Parokiani. Semina katika Jumuiya zote kuhusu Sakramenti ya ndoa, ubatizo na Sakramenti zote kwa ujumla na wajibu wa utoaji wa zaka.  Semina ya VIWAWA. Semina ya WAWATA. Utoaji huduma kwa wasiojiweza kwa kuwatembelea na kuwapa sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Mpako Mtakatifu wa Wagonjwa. Ufundishaji wa Dini shuleni.

B: Mafanikio

Kiroho: Kwa kipindi cha mwaka mzima tumebatiza watu wazima wapatao 27 na watoto wachanga 169 na leo waamini 88 wamepokea sakaramenti ya Kipaimara. Kama Parokia tunamshukuru Mungu kwani ndoa 62 zimebarikiwa. Hakika haya ni mafanikio makubwa sana kwetu na kanisa kwa ujumla. Tunazidi kuwaombea kwa Mungu wale ambao wanaishi pamoja bila sakramenti ya ndoa, Mwenyezi ailainishe mioyo watambue ubaya wa dhambi na wabadilike na kuishi maisha ya neema. Pia tutaendelea kuwaelimisha kwa semina na mahubiri kila mara huenda Mungu akajipatia utukufu katika watu hawa.
Maendeleo

Zipo shughuli za kimaendeleo tunazozifanya kwa sasa katika Parokia yetu, Kwanza tumefanikiwa kujenga nyumba ya mapadre ambayo ilibarikiwa na kuzinduliwa rasmi na Mhashamu Baba Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya alipofanya ziara ya Kichungaji Parokiani kwetu tarehe 13/08/2017. Aidha tunatarajia kununua samani za ndani katika nyumba hiyo ili mapadre wetu waweze kuhamia hapo mapema iwezekanavyo. Jambo la pili tulilofanikiwa ni kupata eneo katika Kigango cha Mt. Anna kwa ajili ya Ujenzi wa Kanisa Kubwa lenye hadhi ya Parokia. Tatu, tunaendelea na ujenzi wa Kanisa la Kigango Cha Mt. Paulo wa Mtume-Maweni pamoja na choo na ofisi. Nne, katika Kigango cha Mt. Maria de Mathias tumeweza kuweka madirisha ya alluminiam jengo la kanisa na kujenga choo na kusafisha eneo lote la kigango kwa kuondoa vichaka vyote. Tano, katika Kigango cha Mt. Yohane Mbatizaji-Sokoine tumefanikiwa kupata eneo ekari tano kwa ajili ya ujenzi wa kanisa baadaye, kwani eneo walilo nalo kwa sasa ni dogo sana. Waamini wa Parokia ya Kisasa wanajitahidi sana katika kuijenga Parokia yao kwa majitoleo binafsi, harambee, zaka, na michango mbali mbali. Wale wachache wanaosuasua tunajitahidi kuwahimiza katika kutimiza wajibu wao kwa Mungu kwa kanisa.

C: CHANGAMOTO KATIKA PAROKIA

Katika Vigango vyetu vya Maweni na Sokoine asilimia kubwa ya familia wanaishi bila ndoa za Kikristo. Mchanganyiko wa Madhehebu pia unaleta changamoto kubwa ya kiimani katika maisha ya familia. Baadhi ya wazazi kuwakazania watoto wao kupata elimu dunia na kusahau kabisa malezi ya kiroho. Hiyo inapelekea watoto kutohudhuria mafundisho kwa sababu ya masomo ya ziada na hivyo uelewa wao wa mambo ya Mungu kuwa mdogo sana.
Kutokuwa na jengo kubwa la Kanisa linalotoa taswira ya Parokia. Kanisa la sasa katika Kigango cha Mt. Anna limejengwa katika kiwanja ambacho ni makazi ya watu. Ujio wa watu kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania kuhamia hapa Dodoma bado inabaki ni changamoto kwetu kwani bado hatujaweza kuwa na miundombinu ya Parokia ambayo watu hawa wataweza kupata huduma zote muhimu. Makatekista tulio nao bado ni wachache ukilinganisha na idadi ya waamini katika Parokia.

D: FURSA

Pamoja na changamoto hizi, zipo fursa ambazo kama tukizitumia vizuri tunaweza kukabiliana na changamoto hizo.

Raslimali watu. Tunao waamni wenye moyo wa kujitolea kwa shughuli za kanisa na walio tayari kusaidia kwa juhudi zinazofanyika. Kama vile kutoa ushauri, kuandika miradi mbali mbali, na kushiriki kwenye michango mbali mbali.
Tunayo maeneo wawili makubwa (Nzuguni Maweni na Nyumba 300) yanayoweza kutumika kwa uwekezaji. Kama vile Chekechea, Shule ya Msingi au Sekondari, Zahanati au hata maeneo ya mapumziko

E: MALENGO

Matarajio yetu ni kujenga kanisa kubwa ambalo litaweza kukidhi mahitaji ya waamini wetu kwa sasa na baadaye Pia tunaendelea kukamilisha miradi ya ujenzi tuliyoianza tayari. Tunamshukuru Mkuu wa Shirika kanda ya Tanzania na uongozi wa Shirika hapa Tanzania na wanashirika wote kwa kuendelea kushirikiana nasi katika kazi ya uinjilisha Parokiani Kisasa. Bikira Maria Mama wa Damu Azizi ya Yesu-Utuombee.

Ni sisi Wamisionari wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu, Padre Perfect Leiya na Padre Innocent Miku Mallya Pamoja na Viongozi wa H/Walei Parokia

Na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S. Kwa ushirikiano na Radio Mwangaza Dodoma.








All the contents on this site are copyrighted ©.