Lifuatalo ni tamko ambalo limetolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto kuhusu taarifa ya ugonjwa wa Ebola katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na kwamba, watanzania wametakiwa kuchukua tahadhari ili wasije kuambukizwa ugonjwa huu ambao ni wa hatari sana. Hadi sasa Wizara inasema, hakuna mtanzania ambaye amekwisha kuambukizwa ugonjwa huu ambao umethibitishwa kwa kutumia vipimo vya maabara na hadi kufikia tarehe 21 Mei 2017 idadi ya wagonjwa imeendelea kuongezeka hadi kufikia wagonjwa 43 na kati yao 4 wamepoteza maisha na wengine bado wanaendelea kupata matibabu nchini humo.
UTANGULIZI
Ndugu Wanahabari,
Kama tulivyowatangazia kwenye taarifa yetu ya Tarehe 15/5/2017, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ilipata taarifa kuhusu mlipuko wa ugonjwa wa Ebola katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) uliotangazwa na Shirika la Afya Duniani siku ya tarehe 12 Mei, 2017. Ugonjwa wa Ebola umethibitishwa kwa kupitia vipimo vya maabara na hadi tarehe 21 Mei, 2017. Idadi ya Wagonjwa imeendelea kuongezeka na kufikia 43 ambapo kati ya hao wagonjwa 4 walipoteza maisha na wengine wanaendelea kupata matibabu katika vituo mbali mbali vya kutolea huduma za afya nchini humo. Ugonjwa huu umetokea katika Jimbo la North-east Bas-Uele linalopakana na nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR) kukiwa na taarifa za kuenea katika maeneo mengine matano ya jirani yakiwemo Nambwa, Muma, Ngayi, Azande na Ngabatala. Wengi wao wamekuwa na dalili za Homa, Kutapika na Kuharisha Damu pia kutokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili.
Wizara ya Afya ya Kongo ikishirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) imeendelea kutekeleza mikakati ya udhibiti wa ugonjwa huu nchini Kongo, ikiwa ni pamoja na kuanzisha maabara ya upimaji wa ugonjwa huo katika wilaya ya Likati ili kuweza kutambua ugonjwa huu mapema. Aidha, Shirika la Afya Duniani limefanya tathmini ya uwezekano wa ugonjwa huu kusambaa nje ya eneo hilo, na tathmini hii imeonesha kuwa kuna uwezekano mdogo wa ugonjwa huu kusambaa nchi jirani kwa kuwa tayari Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo pamoja na Shirika la Afya Duniani wanaendelea na mikakati ya kudhibiti ugonwa huo.
Hatua zilizochukuliwa hadi sasa na Wizara kufuatia kupatikana kwa taarifa ya Ugonjwa huu huko DRC ingawa hakuna mgonjwa yoyote aliyehisiwa au kuthibitishwa kuwa na virusi vya Ebola hapa nchini hadi wakati huu, nchi yetu inapakana na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,hata hivyo kuna uwezekano wa ugonjwa huu kuingia hapa nchini kutokana na mwingiliano wa watu, hasa wasafiri wanaotoka na kuingia hapa nchini. Kutokana na hali hii wizara inaendelea kuchukua tahadhari ili kuzuia ugonjwa huu usiingie hapa nchini. Hivyo, hadi sasa Wizara imefanya yafuatayo,
Kuanzisha ukaguzi ikiwemo upimaji wa joto la mwili (Thermal Screening) kwa wasafiri wanaotoka au kupitia Jamhuri ya Kongo. Hii ni pamoja na kuagiza mashine 4 za nyongeza kwa ajili ya “Thermal Screening” kwa mipaka ya Horohoro,Mutukula, Rusumo na Sirari ili kuimarisha ufuatiliaji huu. Hadi sasa kuna jumla ya Thermal Scanner 11 na baadhi zipo kwenye matengenezo katika Point of Entries (Songwe Airport, Tunduma, Namanga, Tarakea, Kabanga, Murongo, Kigoma sea port, Kigoma Airport, Manyovu, Mabamba, Mwanza Airport na JNIA)
Kuanzisha rejesta ya kurekodi wasafiri ambao watakuwa wametoka katika Jamhuri ya Kongo ili kuweza kuwafuatilia kwa karibu iwapo watapata dalili za ugonjwa huu. Aidha Pamoja na rejesta, wasafiri watakaotoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo watapaswa kujaza fomu maalamu ili kuweza kupata taarifa zao na ili kurahisisha ufuatiliaji wa wasafiri hawa iwapo wataonesha dalili za ugonjwa huu. Kuendelea kutoa elimu kwa jamii kupitia mabango, vipeperushi, Radio, Televisheni na mitandao ya kijamii. Elimu ya ugonjwa huu inatolewa pia kwa njia ya kupiga simu kwenda namba 117. Huduma hii inatolewa bila malipo kwa mitandao yote. Wizara inaendelea kufanya kazi kwa ukaribu na Shirika la Afya Duniani (WHO), US-CDC pamoja na mashirika mengine ya Kimataifa kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu za Kimataifa na Kitaifa. Kwa sasa Wizara inapokea taarifa ya kila siku ya Ugonjwa wa Ebola, na kuzifanyia tathmini kwa karibu na kutoa maelekezo kwa Maofisa Mbalimbali wakiwemo Waganga wakuu wa Mikoa ili kuona jinsi hali inavyoendelea na kuboresha mipango yetu.
Hitimisho
Wananchi wanashauriwa kutokuwa na hofu na waendelee kuchukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa huu. Aidha Wizara inaendelea kusistiza kuwa hadi sasa hakuna mtu yeyote aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa huu hapa nchini. Vilevile, Wizara inaendelea kushirikiana na sekta mbalimbali katika kuimarisha ufuatiliaji na kutekeleza mikakati ya kudhibiti ugonjwa huu ili usiingie hapa nchini. Pia Wizara itaendelea kutoa taarifa pamoja na Elimu ya Afya kwa Jamii kadri itakavyohitajika.
All the contents on this site are copyrighted ©. |