2017-05-18 15:40:00

Papa Francisko "kuchonga" kwa faragha na Maaskofu tarehe 22 Mei 2017


Baraza la Maaskofu Katoliki Italia kuanzia tarehe 22 Mei 2017 majira ya saa 10: 30 jioni kwa saa za Ulaya hadi Alhamisi tarehe 25 Mei 2017 litakuwa linaadhimisha mkutano wake wa 70 utakaofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano ya Sinodi ulioko mjini Vatican. Mkutano huu utafunguliwa rasmi na Kardinali Angelo Bagnasco ambaye anamaliza muda wake wa uongozi kama Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia. Baba Mtakatifu anatarajiwa kutoa neno na baadaye kujadiliana na Maaskofu wenzake kwa faragha, mambo msingi katika maisha na utume wa Kanisa.

Kardinali Angelo Bagnasco, Jumanne tarehe 23 Mei 2017 atazungumza na waandishi wa habari. Hii ni siku ambayo pia Maaskofu watafanya uchaguzi mkuu ili kupata Rais wa Baraza atakayechukua nafasi ya Kardinali Bagnasco anayeng’atuka kutoka madarakani. Mada kuu inayoongoza mkutano mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia kwa wakati huu ni “Vijana, ili kukutana katika imani”. Maaskofu watatumia fursa hii pia kufanya maandalizi ya kina kwa ajili ya maadhimisho ya Juma la Mafundisho Jamii ya Kanisa litakalo adhimishwa mjini Cagliari kuanzia tarehe 26- 29 Oktoba 2017.

Maaskofu pia watapitia baadhi ya vipengele vya sheria kuhusu uongozi wa Mahakama za Kanisa. Jumatano tarehe 24 Mei 2017 majira ya saa 2:30 asubuhi kwa saa za Ulaya, Baraza la Maaskofu Katoliki Italia litaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Alhamisi, tarehe 25 Mei 2017, Baraza la Maaskofu Katoliki Italia litazungumza na waandishi wa habari mjini Vatican kwenye Ukumbi mdogo wa Paulo VI kama kilele cha maadhimisho ya Mkutano wa 70 wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.