2017-05-18 15:24:00

Familia ya Mungu Jimbo kuu la Genova, kutembelewa na Papa 27 Mei 2017


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 27 Mei 2017 anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji Jimbo kuu la Genova, Kaskazini mwa Italia ambako atakutana na kuzungumza na ulimwengu wa wafanyakazi wanaokabiliana na changamoto nyingi katika maisha yao! Atakutana na kuzungumza na wakleri, watawa na viongozi wa dini na madhehebu ya Kikristo Jimboni humo. Kama sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Vijana, Baba Mtakatifu atakutana na kuchonga pamoja na vijana, ili kuwatangazia Injili ya furaha na matumaini! Ataungana na wafungwa kwa njia ya televisheni na hatimaye, kusalimiana nao!

Baba Mtakatifu Francisko atakula chakula cha mchana maskini, wakimbizi, wahamiaji na wafungwa. Jioni kabla ya maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu atakwenda kuwasalimia watoto wagonjwa waliolazwa kwenye Hospitali ya Watoto ya “Giannina Gaslini” mjini Genova. Mwishoni, jioni, Baba Mtakatifu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Kennedy na hatimaye, kurejea tena mjini Vatican kuendelea na shughuli zake, kwani Jumapili, tarehe 28 Mei 2017, Kanisa litakuwa linaadhimisha Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni sanjari na Siku ya 51 ya Upashanaji Habari Duniani ambayo kwa mwaka huu inaongozwa na kauli mbiu “Usiogope, maana mimi ni pamoja nawe”. Kutangaza matumaini na imani katika nyakati hizi”.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.