2017-05-11 07:22:00

Papa Francisko: Ninakuja kuwashirikisha Injili ya matumaini na amani!


Baba Mtakatifu Francisko anafanya hija ya kitume kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Fatima kuanzia tarehe 12 – 13 Mei 2017. Hija hii inaongozwa na kauli mbiu “Papa Francisko mjini Fatima 2017 pamoja na Bikira Maria kama mahujaji wa matumaini na amani”. Kama sehemu ya maandalizi haya, Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe wa matumaini kwa familia ya Mungu nchini Ureno akionesha furaha ya kutaka kukutana nao kwenye nyumba ya Mama wa Mungu. Anatambua kwamba, hata wao wangependa awatembelee nyumbani, kwenye familia, vijijini na mijini kwao, mwaliko umemfikia, lakini kwa bahati mbaya, haitawezekana.

Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru viongozi kwa uelewa wao, unaomwezesha kukita hija hii ya kitume nchini Ureno katika tukio maalum, kwa kutembelea Madhabahu ya Bikira Maria wa Fatima, mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuonana naye mbele ya Bikira Maria. Kwa mavazi ya mchungaji mkuu ambayo amemkirimia, Baba Mtakatifu anasema, angependa kwenda kumzawadia shada la maua mazuri zaidi ambayo Yesu amemkabidhi ili aweze kuyatunza; yaani: watu wote duniani waliokombolewa kwa Damu yake azizi, bila kumbagua wala kumtenga mtu yeyote! Ili kutekeleza azma hii, Baba Mtakatifu anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuungana naye: kiroho na kimwili; jambo la msingi hapa si umbali bali nia ya kuwa na roho moja katika shada lake la maua, “shada la maua ya dhahabu”. Kwa njia hii wote kwa pamoja wanakuwa ni moyo mmoja na roho moja, atawakabidhi kwa Bikira Maria na kumwomba amnong’onezee kila mmoja wao akisema “Moyo wangu safi usiokuwa na doa, uwe ni kimbilio lako, safari itakayokupeleka kwa Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, kauli mbiu ya “Pamoja na Bikira Maria kama mahujaji wa matumaini na amani” inafumbata programu nzima ya wongofu wa ndani. Baba Mtakatifu anawashukuru na kuwapongeza kwamba, wanaendelea kujizatiti katika maadhimisho haya kwa sala itakayohitimisha matukio muhimu sana yaliyojitokeza katika kipindi cha Miaka 100 iliyopita. Hii ni nafasi kwa waamini kupanua nyoyo zao ili kujiandaa kupokea zawadi ya Mungu. Baba Mtakatifu anawashukuru kwa sala na sadaka wanazotoa kwa ajili ya maisha na utume wake, ni muhimu sana, kwani anajitambua kuwa ni mdhambi kati ya wadhambi “ni mtu mwenye midomo michafu anayeishi kati ya watu wenye midomo michafu. Sala anasema Baba Mtakatifu, inayaangazia macho yake ili kuweza kuwaangalia wengine kama jinsi ambavyo Mwenyezi Mungu anawaangalia; kuwapenda wengine, kama jinsi ambavyo Mwenyezi Mungu anavyowapanda. Mwishoni, Baba Mtakatifu anasema kwa jina la Mwenyezi Mungu anakwenda nchini mwao kwa furaha ili kuweza kushirikishana Injili ya matumaini na amani. Baba Mtakatifu anawapatia wote baraka yake ya kitume!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.