2016-12-20 10:11:00

Waamini wanahimizwa kuadhimisha Mafumbo ya Huruma ya Mungu!


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, neno Huruma ya Mungu limesika mara nyingi sana masikioni mwako, na  bado linaendelea kukujia, ila leo linakujia katika ujumbe  mzito uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko , ambapo analeta kwetu mwito wa kusherekea huruma ya Mungu. Hapa anasema awali ya yote tunaitwa kusherekea huruma ya Mungu, na kwa hilo tutapata utajiri wa neema  zitokanazo na huruma hii ya Mungu. Katika waraka wake wa kitume “Misericordia et misera” yaani Huruma na amani, Baba Mtakatifu anasema,  Huruma ya Mungu hujitokeza kiundani kabisa hasa katika adhimisho la Liturujia, anatuambia toka mwanzo wa adhimisho la Ekaristi Takatifu, Huruma  ya Mungu hujitokeza kwa wingi  hasa katika mwitikio na ushiriki wa sala za waamini na Mungu mwenyewe.

Ujumbe  huu, Huruma na amani  ya kimungu,  ni ule mwitikio utokao kwa Mungu  na Mwanaye Yesu Kristo. Ambapo amani hii ni utulivu wa ndani  wa moyo na roho  ambao umwadhimisha  Kristo  ndani yake bila  kujali  mazingiza au  watu. Baba  Mtakatifu anatuambia,  amani hii tunaweza kuipata  zaidi  katika adhimisho  la Liturujia takatifu , pamoja na Sakramenti nyingine  za kanisa  ikiwemo  Sakramenti ya upatanisho,  kwani  Huruma na amani  ni  matokeo  ya  muunganiko  wa kiundani  baina ya  mwamini  na Mungu Mwenyezi   kupitia sadaka  ya Yesu Kristo Msalabani. Mtakatifu Paulo  anatuambia, amani  iletayo furaha ya ndani,   yapatikana tu kwa  wale  wanao mwamini  Kristo (Warumi 15:13), mwamini yeyote anayeguswa  na huruma  na amani ya Mungu  atapata  kutambua  mamlaka  ya Kimungu  na hivyo,  kumrudishia Mungu  sifa na shukrani,  kwani Mungu ndiye atujaliae,  huruma na amani ya kweli.

Adhimisho la huruma ya Mungu  hupata utulivu wake katika Ibada takatifu , ambapo Fumbo la Pasaka uadhimishwa , na chanzo cha wokovu wa mwanadamu  huonekana  katika historia na zaidi katika ulimwengu mzima.  Baba  Mtakatifu anatuambia, Kila neno katika adhimisho la Fumbo la Ekaristi takatifu lina umaana  wa huruma ya Mungu,  huruma iletayo amani na furaha moyoni. Na hii ndiyo ile   amani tuipatayo  kupitia  sadaka  ya Yesu  Msalabani , ikituunganisha  katika Amani ya Mungu  Baba, na   amani  hii  itokayo kwa Mungu isingwezekana  bila huruma ya Mungu. Katika hilo twashuhudia ukuu wa Huruma ya Mungu katika maisha ya mwanadamu.  Hivyo, mwanadamu aliyeumbwa katika hali ya upendo na amani ya kimungu, analo jukumu la kuishi hii amani ya kimungu na pia kuieneza kwa wengine kama ushuhuda wa imani tendaji!

Baba  Mtakatifu Francisko anatualika kuwa na muunganiko wa ndani na Mungu na huko ndiko kujipatia  amani nafsini mwetu. Na amani hii itapatikana hasa katika maisha ya Sala na maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa. Katika hilo, adhimisho la Ekaristi  takatifu lamjia mwanadamu  kwa   hadhi ya juu kabisa katika kumpatia mwanadamu amani na furaha moyoni.  kwani  ni katika tendo hili, tunakutana na kuunganika na sadaka ya Yesu msalabani, ambaye kwa kifo na ufufuko wake  tumepatanishwa na Mungu na hivyo kuinuliwa na kupewa hadhi ya kuitwa wana wa Mungu. Ninakutakia, heri na baraka, jitahidi kuwa kweli ni chambo cha amani na furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake!

Kutoka studio za Radio Vatican ni mimi, Padre, Agapiti Amani, ALCP/OSS.








All the contents on this site are copyrighted ©.