2016-12-09 15:19:00

Rais Magufuli na Watazania waadhimisha miaka 55 ya Uhuru wa Tanzania Bara


 9 Desemba  Rais  John Magufuli  aliongoza watanzania katika kilele cha maadhimisho ya Miaka 55 ya Uhuru wa Tanzania Bara, yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, ikiwa ni mara yake ya kwanza kushiriki sherehe hizo.

Kaulimbiu katika maadhimisho hayo ni “Tuunge mkono jitihada za kupinga rushwa na ufisadi na tuimarishe uchumi wa viwanda kwa maendeleo yetu.”

Maadhimisho hayo yalifanyika kwa mara ya kwanza tangu Dk Magufuli kuingia madarakani kutokana na mwaka jana kuzisitisha na kutaka kuadhimishwa kwa kufanya usafi katika maeneo mbalimbali nchini;  aliagiza fedha zilizokuwa zimetengwa kwa maadhimisho hayo zaidi ya Sh bilioni nne kutumika kufanya upanuzi wa barabara ya Mwenge hadi Morocco jijini Dar es Salaam yenye urefu wa kilometa 4.3 kwa kuongeza njia mbili za barabara za lami.


Katika maadhimisho hayo yalihudhuriwa na marais wa nchi jirani na viongozi wastaafu. Wakati sherehe  zilipambwa na gwaride la heshima lililoandaliwa na Vikosi vya Ulinzi na Usalama ikiwemo Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Polisi na Magereza.Vilevile kulikuwa na maonesho ya kwata la kimya kimya pamoja na makomandoo wa JWTZ, burudani za vikundi vya muziki wa kizazi kipya na kizazi cha zamani pamoja na ngoma za asili kutoka mikoa ya Mbeya, Pwani, Lindi na Zanzibar.


Akikaririwa katika maadhimisho hayo, Spika wa Bunge mstaafu, Pius Msekwa aliwataka Watanzania kusherehekea sikukuu hiyo kwa kumuenzi Rais wa Kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere kwa kuzingatia na kuendeleza misingi aliyoacha ambayo marais wote waliomfuata waliisimamia.
Msekwa ambaye pia aliwahi kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), alisema katika maadhimisho hayo ni vema kumkumbuka Nyerere na wenzake walioshiriki kupigania kwa kutambua kuwa haukuja kama mvua na bila wao katika nyakati hizi hali ingekuwaje?


Aidha alisema ni vema kuangalia kwa jinsi alivyopambana na changamoto mbalimbali wakati wa kugombania uhuru na jinsi alivyokuwa akitumia busara na kuona mbali kuwashauri wenzake na kutoa mfano katika moja ya kikao, wenzake walishauri kususia, lakini yeye aliona mbali kwa kuwataka kushiriki kwani kususia kwao kungetoa mwanya kwa wakoloni kuzidi kuwatawala.


Na Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican Inaungana na watanzania wote walioko ndani na nje ya nchi kutakiana Baraka na Amani ya nchi  na kumuenzi Mwasisi wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

 








All the contents on this site are copyrighted ©.