2016-11-29 08:12:00

Kanuni za kuzingatia kuhusiana na vitega uchumi vya watawa


Kongamano la Pili la Kimataifa kuhusu uchumi, lililokuwa limeandaliwa na Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume lililofunguliwa hapo tarehe 25 Novemba 2016 limefungwa rasmi, Jumapili tarehe 27 Novemba 2016 kwa kutoa mwongozo unaopaswa kufanyiwa kazi na watawa kwa siku za usoni ili kuendelea kuwa waaminifu kwa karama za Mashirika yao, huku wakiwa na mwelekeo mpana zaidi kuhusiana na masuala ya kiuchumi.

Kardinali Joao Braz de Aviz, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume amewakumbusha watawa kwamba, wanapaswa kuwa makini zaidi na masuala ya kiuchumi, kwa kuhakikisha kwamba, wanatumia weledi, ujuzi, mang’amuzi na historia ya Mashirika yao, ili kuendelea kuwa ni mashuhuda wa tunu msingi za Kiinjili hata katika masuala ya kiuchumi. Lengo ni kuendelea kuwa waaminifu kwa karama za Mashirika haya, lakini kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kuangalia changamoto zinazoendelea kujitokeza katika masuala ya uchumi na maendeleo pamoja na athari zake kwa utu na heshima ya binadamu.

Kardinali Joao Braz de Aviz anakaza kusema, Mashirika ya Kitawa yamewekeza kwa kiasi kikubwa katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu ya binadamu. Hapa kuna haja ya kuwa makini na Sheria za Kanisa pamoja na Sheria za Nchi husika; mambo ambayo yanahitaji kufanyiwa upembuzi yakinifu ili kuweza kuleta mabadiliko yanayokusudiwa kadiri ya Mafundisho ya Kanisa kwa wakati huu. Hapa maamuzi ya sera, mikakati na utekelezaji wake yanapaswa kufanywa na Shirika zima na wala si maamuzi ya mtu mmoja au kikundi cha watu wachache, ili kuweza kujenga uwajibikaji wa pamoja.

Ikumbukwe kwamba, rasilimali fedha na watu ni mali ya Kanisa kwa ajili ya kusaidia mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Wajumbe wa kongamano baada ya kujadili kwa kina na mapana kuhusu: karama, uaminifu na mwelekeo mpya wa masuala ya kiuchumi, waliunda kikosi kazi kilichokuwa kinawajumuisha: wanasheria, wachumi na wataalam mbali mbali ili kuweza kutoa mapendekezo ambayo yatawasilishwa kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya kuyafanyia kazi kwa siku za usoni katika sekta ya afya, elimu na maendeleo endelevu sehemu mbali mbali za dunia!

Kongamano hili ni matunda ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, uliowachangamotisha watawa kuwa kweli ni cheche za matumaini kwa kusikiliza Neno la Mungu pamoja na kufikiri, kuamua na kutenda mintarafu dhana ya Sinodi inayoendelea kushika kasi katika maisha na utume wa Kanisa, ili kuwa na maamuzi fungamanishi. Nadhiri za kitawa anasema Sr. Nicla Spezzati, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume, ni kioo cha maisha, utume na mahusiano yao na walimwengu mintarafu karama za Mashirika yao. Huu ni mwaliko wa kujenga na kuimarisha mshikamano wa dhati na maskini pamoja na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Watawa wawe mstari wa mbele kulinda na kutetea utu, heshima, haki, ustawi na mafao ya wengi kwa njia ya ushuhuda wa maisha na utume wao. Utajiri wa karama na rasilimali fedha na watu, visaidie kupambana na baa la umaskini na changamoto zinazowakabili maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.

Askofu mkuu Josè Rodriguez Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume amewasilisha mambo makuu matano yanayopaswa kuzingatiwa na Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume kuhusiana na masuala ya uchumi na vitega uchumi. Mosi, Uaminifu kwa karama maana yake ni kuendeleza utume pamoja na kuwa na matumizi sahihi ya rasilimali ya Shirika kwa ajili ya huduma kwa karama.

Pili, utunzaji bora wa mali ya Kanisa. Watawa wanapaswa kuwa makini katika kulinda mali ya Kanisa ili kuweza kujitosheleza katika mahitaji yao msingi pamoja na maendeleo ya Shirika kwa siku za usoni. Tatu ni mwendelezo wa vitega uchumi vya Shirika hapa ieleweke kuwa ni mchakato wa kufanya upembuzi yakinifu ili kuhakiki pamoja na kuwa makini ili kuangalia ikiwa kama miradi husika inaweza kujiendesha, kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa karama pamoja na uwiano mzuri wa kiuchumi.

Nne, uwajibikaji wa kutoa taarifa: kwa kuonesha malengo na mbinu mkakati zitakazotumiwa ili kufikia malengo husika kwa kuzingatia: Sheria za Kanisa na Sheria za nchi pamoja na kuhakikisha kwamba, taarifa zinatolewa kwa wakati muafaka kuhusu utekelezaji wa miradi na vitega uchumi vilivyopo! Tano ni ufukara, yaani kutumia rasilimali vitu na fedha kwa lengo na nia husika pamoja na kuhakikisha kwamba, wanaondokana na dhana ya kuwa ni wamiliki wa mali husika, bali wasimamizi na waratibu wa rasilimali ya Kanisa kwa ajili ya kusaidia mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Askofu mkuu Josè Rodriguez Carballo anahitimisha kwa kusema kwamba, kuna vigezo vingine vinavyoweza kuongezwa kutokana na hali halisi ya Shirika husika, vitega uchumi na kazi zinazoendeshwa mintarafu mahali na mazingira; sheria zilizopo na utekelezaji wake.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.