2016-11-28 15:52:00

Itengenezeni njia ya Bwana, yanyoosheni mapito yake!


Ndugu yangu, twasikia kwa mbali sauti ya mtu aliyaye nyikani na huyu si mwingine bali ni  Yohana Mbatizaji, sauti hii ya mtu aliyaye nyikani yatutangazia, kutimia kwa wokovu wetu kama ilivyo  kwisha nenwa  na Manabii. Hii ni sauti ya maandalizi,  maandalizi ya kumpokea mwokozi. Sauti hii yatuambia mwokozi amekaribia na kipindi cha kumsubiri kimekaribia, kipichi hicho  ni  kipindi cha majilio. Ni kipindi cha matumaini kwani mwokozi yu karibu, na ukamilifu wa ahadi ya Bwana unakaribia, na furaha ya mwanadamu inaongezeka.

Habari hizi za ujio wa Kristo, ni habari zilizokwisha nenwa na manabii toka enzi. na kuzaliwa kwa Yesu kwadhihirisha na kudhibisha utimilifu huu, yaani utimilifu wa ahadi ya Mungu, ukweli wa manabii  na tabiri zao.  Hebu kwa ufupi tangalie baadhi  ya tabiri hizo za kinabii, na utimilifu wake, ili wote tupate kuamini ya kuwa Kristo ni Bwana, na kila goti litapigwa kwa ajili yake.

Yapata miaka 750, KK. Nabii Isaya alinena maneno haya;  “Haya basi tazama  msichana  Bikira atachukuwa Mimba na atajifungua mtoto wa Kiume na kumwita jina lake Emmanueli. (Rej. Is  7:14), unabii huu unatimia sasa katika kuzaliwa Bwana, kama Luka Mwinjili  anavotuambia;  Siku yake ya kujifungua ikawadia  akajifungua mtoto wake wa kwanza wa kiume, akamvika nguo zake za kitoto akamlaza horini  kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni (Lk 1:6-7).

Mnamo mwaka wa 587-542, KK, Nabii  Mika anatuandikia utabiri mwingine, kuhusu  kuzaliwa kwa Yesu. Kwamba  atazaliwa wapi  na katika mji gani’ kwani  anasema ‘ mwenyezi Mungu, Mungu asema; “lakini wewe  Bethlehemu   katika  Efratha, wewe ni mdogo tu kati  ya jamii ya Yuda, lakini kwako kutatoka mtawala  atakayetawala  juu ya Israeli  kwa niaba yangu (Mik  5:1ff.)  Utabiri huu unatimia katika maandiko ya Mwinjili Luka anayetuambia; “alikwenda mjini Bethlehemu  mkoani Yudea alikozaliwa mfalme Daudi , walipokuwa huko siku yake ya  kujifungua  ikawadia. (Rej. Lk  2:4-7. Yesu anazaliwa kweli Bethlehem kama ilivyonenwa na nabii  Mika.

Mnamo mwaka wa 742  KK, Nabii Isaya anaendelea kutabiri ;  “maana mtoto amezaliwa   kwa ajili yetu, tumepewa mtoto wa kiume,  naye atapewa mamlaka ya kutawala (Rejea Is  9:6) Unabii huu unatimia kama Luka mwinjili atuandikiavyo.. kwa maana leo hii katika mji wa Daudi , amezaliwa mwokozi kwa ajili yetu ndiye Kristo Bwana.  (Rej. Lk  2:11-12).

Unabii mwingine ni huu; “Tazama namtuma mjumbe  wangu   na ataindaa njia kabla yangu  Is  40:3,  utabiri huu ulinenwa na Nabii Isaya  yapata miaka 700  KK, na  unatimia kwa Sauti ya Yohane mbatizaji  aliyehubiri ujio wa Bwana,  akisema  Sauti ya mtu aliaye jangwani, mtayarishieni Bwana njia yake, nyosheni barabara zake,  na  akaendelea kuhubiri watu watubu  na kubatizwa,  ili Bwana awasemehe dhambi zao. (Mk  1:3-4). Na Yesu  alipokuja, Yohane Mbatizaji akamtambulisha kwetu  kwa maneno haya..” Huyu ndiye mwanakondoo wa Mungu,   aondoaye dhambi za ulimwengu. Huyu ndiye nilieongea juu yake  niliposema  ‘ baada yangu anakuja mtu mmoja aliye mkuu kuliko mimi.  (Rej. Yn  1:29-30.) Yohane  Mbatizaji  anakuwa mmojawapo wa manabii wanao hubiri  katika  ukaribu sana  ujio wa Kristo.  Yohani  mbatizaji  ndiye  Sauti  ya mtu aliaye nyikani, aliyenenwa na nabii Isaya   Takribani miaka 720  KK.

Ndugu yangu  sasa utabiri wa manabii umetimia, malaika anatumwa kwa msichana Bikira na anampa habari ya kuzaliwa Bwana, naye huyu Bikira anajibu  ‘mimi ni mtumishi wa Bwana nitendewe ulivyonena  Lk1:38.  Hivyo hili ni tukio kubwa na la ajabu kuwahi kutokea Dunia hii, ambapo mwana wa Mungu anajivika ubinadamu wetu katika   tumbo la Mama Bikira Maria, na hivyo tunaona utimilifu wa wazo la Mungu katika kumkomboa mwanadamu, kwani toka kuumbwa kwa ulimwengu na kwa anguko la kosa la Adamu na Hawa la kutotii, Mungu alianza kazi ya kumkomboa mwanadamu hatua kwa hatua, na hatua hii inafikia  utimilifu wake katika Yesu. Kwa kuzaliwa Yesu  tunatambua huruma na upendo wa Mungu kwa mwanadamu, na kupitia Yesu  wote tunafanyika  wana wa Mungu na waridhi wa ufalme wa mbinguni. Kwa jambo hili kubwa tumrudishie Mungu sifa na shukrani.

Kipindi hiki cha majilio ni kipindi muhimu cha  kuangalia na kuchunguza  ndani ya mioyo yetu na kuona tena ni kwa namna gani tusimamapo mbele ya Mungu. Hivyo twatakiwa kumrudishia Mungu sifa na shukrani kwa  kuishi ki- ukweli na kiualisia kama wafuasi wa kweli wa Kristo, na kama hatujafanya hivyo wakati ni sasa   wa kubatilisha mioyo yetu  na kuacha ubaridi wa Imani, na mengine yanayofanana na hayo; ili  kupata kumgeukia Bwana na  kuishi ukweli katika njia iendayo mbinguni. Mungu anatuita tuyafanye haya leo,  na huku ndiko kuitikia mwito wa sauti ya Yehoni mbatizaji, asemayo; “Tubuni, muache dhambi zenu, mmgeukie Mungu; kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia.

Kutoka katika Studio za Radio Vatican, ni mimi wako Padre, Agapiti Amani, ALCP. OSS








All the contents on this site are copyrighted ©.