2016-11-09 07:21:00

Familia ya Mungu nchini Zambia shikamaneni kwa pamoja!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, Jumatatu, tarehe 7 Novemba 2016 amekutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia kwa kugusia kwa namna ya pekee kabisa: hali ya maisha na utume wa Kanisa Katoliki nchini Zambia; umuhimu wa kujikita katika ushuhuda wa furaha ya Injili; changamoto za Uinjilishaji wa watu na ujasiri wa kusonga mbele katika maisha na utume wa Kanisa licha ya changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza.

Kardinali Filoni anasema, hija yake ya kitume nchini Zambia, imemwezesha kukutana na wawakilishi wa familia ya Mungu, ili kuonesha uwepo wa karibu wa Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wa Kanisa. Anawashukuru Maaskofu kwa moyo wa upendo na ukarimu waliomwonesha tangu alipowasili nchini Zambia na kuwapongeza kwa majitoleo yao katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa nchini Zambia, limebahatika kuwa na taasisi mbali mbali za huduma za kijamii katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Kanisa linaendelea kupanuka kutokana na ongezeko la idadi ya Parokia, Miito ya Kipadre na Kitawa. Lakini pia familia ya Mungu nchini Zambia, inakabiliwa na hali mbaya ya hewa iliyopelekea ukame wa kutisha; ukosefu wa fursa za ajira, umaskini pamoja na ongezeko kubwa la maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi. Zambia bado inakabiliwa na changamoto ya ukabila, changamoto kwa wananchi wa Zambia kujikita katika mchakato wa ujenzi wa umoja na mshikamano wa kitaifa.

Waamini nchini Zambia wanahamasishwa kuwa kweli ni vyombo na mashuhuda wa huruma na upendo wa Mungu unaobubujika kutoka katika furaha ya Injili, kiini cha uinjilishaji, kinachomwezesha mwamini kukutana na Kristo Yesu, tayari kufanya mabadiliko katika maisha yake. Uinjilishaji wenye mvuto na mashiko kwa njia ya huduma ya upendo kwa maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii ndio mwelekeo wa Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Kristo. Kanisa linapaswa kuwa ni chombo cha matumaini kwa wale waliokata tamaa ya maisha.

Hivi karibuni, Kanisa limeadhimisha Jubilei ya miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka kuhusu Kazi za Kimissionari za Kanisa “Ad Gentes” na sasa Zambia inaadhimisha Jubilei ya miaka 125 ya uwepo na utume wa Kanisa Katoliki nchini humo. Haya ni matunda ya kazi kubwa iliyotekelezwa na Wamissionari wa Afrika waliojisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu nchini Zambia.

Juhudi hizi zilikwenda sanjari na mchakato wa Utamadunisho, leo hii, Injili imeweza kuingia na kukita mizizi yake katika maisha, tamaduni, mila na desturi za wananchi wengi wa Zambia, changamoto ni kuendelea kusimama kidete ili kukuza na kudumisha ari na moyo wa kimissionari. Familia ya Mungu katika ujumla wake, inayo changamoto kubwa ya kuhakikisha kwamba kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo wanatangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu inayofumbatwa katika tunu msingi za Kiinjili na maisha ya ndoa na familia; ili kweli familia ziweze kuwa ni Kanisa dogo la nyumbani, madhabahu ya Injili ya uhai yanayojikita katika uaminifu, udumifu na malezi kwa watoto.

Hii ni changamoto kwa familia ya Mungu nchini Zambia kwa mfano wa mashahidi wa imani kutoka Barani Afrika, kuhakikisha kwamba, inakuwa ni chombo na shuhuda wa matumaini na huruma ya Mungu; ili kukuza na kudumisha majadiliano katika ukweli na uwazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Dhamana ya kwanza kabisa kwa Maaskofu ni kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa watu wote. Juhudi hizi hazina budi kuungwa mkono na matumizi bora zaidi ya vyombo vya mawasiliano ya jamii sanjari na kusimama kidete kulinda na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.

Maaskofu wanapaswa kuhakikisha kwamba, wanajisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuhamaisha miito mitakatifu pamoja na kukazia majiundo awali na endelevu kwa Majando kasisi nchini Zambia. Dhamana hii inatekelezwa kwa Maaskofu kutoa walezi bora na wenye sifa za: kiutu, kiakili, kiroho na kichungaji. Mapadre walezi waandaliwe vyema, ili kuwawezesha kutekeleza dhamana na wajibu wao barabara. Maaskofu wawe ni vyombo na wajenzi wa umoja, upendo na mshikamano wa Kanisa. Waendelee kushirikiana kwa karibu zaidi na wanasiasa kwa ajili ya mafao ya wengi. Wakleri wawe makini wanapojihusisha na masuala ya kisiasa.

Maaskofu waoneshe heshima na upendo kwa Mapadre wao; kamwe wasikubali kumezwa na malimwengu au kutumbukia katika ulevi wa kupindukia. Wawe na jicho la huruma na mapendo kwa wale walioathirika kwa ugonjwa wa Ukimwi. Maaskofu wawawezeshe Mapadre wao kiuchumi sanjari na kudumisha maisha ya kitawa katika majimbo yao, daima wakionesha ari na moyo wa huduma kwa familia ya Mungu nchini Zambia. Maaskofu wahakikishe wanakuwepo Majimboni mwao kwa ajili ya huduma kwa familia ya Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.