2016-09-27 15:13:00

Papa: ahimiza kushinda huzuni kwa maombi na si kwa ulevi wa dawa au pombe


Baba Mtakatifu Francisko Mapema Jumane hii akiongoza Ibada ya Misa katika Kanisa dogo la Mtakatifu Marta ndani ya Vatican, alizungumzia juu ya huzuni au mateso ya kiroho kutokana na misukosuko ya maisha kama maradhi na majanga. Alihoji  nini hasa kinachotokea moyoni wakati tunapokumbwa na  fadhaa ya  kiroho?  Homilia ya Papa ilitafakari kwa kina somo kutoka kitabu cha Ayubu, na kusistiza umuhimu wa maombi na sala ili kuyashinda yanayotia giza rohoni. Katika Ibada hii, pia Papa  alifanya rejea katika historia ya maisha ya Mtakatifu Vincent de Paul , na pia aliwakumbuka  Masista wa Mtakatifu Vincent , Mabinti wa Upendo , wanaofanya utume wao katika Jengo la Mtakatifu Marta la ndani ya Vatican,  anakoishi Papa Francisko.   

Mafundisho ya Papa Francisko , yaliutazama kwa kina wakati huu wa  shida na mateso, kama ilivyokuwa kwa  Ayubu , ambaye alipoteza kila kitu chake , si mali tu lakini pia watoto , hali iliyomletea kupoteza imani na kujiona kama amelaaniwa na Bwana.  Papa alilinganisha wakati huu mgumu kwa Ayubu, na uzoefu wa maisha yetu , ambamo katika vipindi fulani pia tunakabiliwa na hali hiyohiyo ngumu na kukatiksha tamaa , ambamo tunaona kama hatuwezi tena kusonga mbele na maisha, ambamo  roho husongwa na mfadhaiko mkubwa  mbele ya uso wa Mungu, na kuwa sawa na mtoto mdogo aliyepoteza matumaini mbele ya baba yake. Kama pia ilivyokuwa pia kwa Nabii  Yeremia, alivyomkasilikia Mungu.  

Papa ameutafakari udhaifu huu wa kiroho alisema kwamba hutokea kwa kila mmoja wetu, katika hali mbalimbali wengine kwa nguvu zaidi na wengine katika kishindo cha kawaida,  lakini kwa vyovyote vile,  huleta giza moyoni , moyo kutaka tamaa , kutoona tena faida ya kuishi , kutamanai kufika mwisho wa safari ya maisha  kwa  hasira nyingi na mawazo mengi  na kwa huzuni kubwa. Hali kama hizi Papa Francisko amesema , huidhoofisha roho na kupata  hisia za kuangamia, kama vile hakuna tena maana ya kuishi ,mtu akiona heri kufa kuliko kuishi , kama kilivyokuwa kilio cha Ayubu.

Papa alieleza na kuhoji kumbe basi tufanye nini wakati tunapokutana na changamoto kama hizi , tunapopambana na hali ya kutia giza moyo , kupitia matukio mbalimbali katika maisha , kwa mfano majanga kwa familia, au  magonjwa, jambo jingine lolote linaloshusha imani yetu? Jambo linalotukaba kiasi cha kukosa usingizi ? je tumezevidoge na kujimaliza au tubobee katika ulevi wa pombe au madawa ya kuelvya ? hivyo vyote havitasaidia kitu.

 Papa ameshauri   jawabu pekee kama ilivyo katika liturujia ya Neno la Mungu kwa siku hii,  ni kuzama zaidi katika   maombi na sala kwa Mwenyezi Mungu. Tunahitaji kuomba, kila wakati usiku na mchana ni  kumlilia Mungu kwa nguvu kama  alivyofanya Ayubu: mchana na usiku, ni kutoa kilio hadi sikio la Mungu lisikie.  

Dawa pekee amesisitiza Papa,  ni maombi. Kugonga kwa nguvu katika mlango wa Bwana na kummiminia matatizo yote , kumwambia, 'Bwana, Bwana , nisaidie naangamia. Maisha yangu  yanaelekea  kuzimu. Papa aliongeza, ni lazima tunapokuwa katika hali ya giza giza la kiroho,  kuomba zaidi na zaidi  na Bwana kwa haki atatenda kulingana na mapenzi yake.

Baba Mtakatifu Francisko ameeleza na kukamilisha kwa kumwomba Bwana, atupatie neema tatu:  neema ya kutambua udhaifu wetu ,  neema ya kuomba tunapokabiliwa na changamoto na neema ya kujua watu wa kuongozana nao  wakati wa mateso au nyakati mbaya za huzuni na mfadhaiko wa  kiroho.  








All the contents on this site are copyrighted ©.