2016-07-29 14:48:00

"No comment"!


Bwana uwahurumie watu wako! Bwana wasamehe kutokana na ukatili huu! Ni maneno ambayo yameandikwa na Baba Mtakatifu Francisko, Ijuamaa, tarehe 29 Julai 2016 kwenye Kitabu cha wageni mashuhuri kwenye Kambi ya mateso na mauaji ya Auschwitz. Katika hali ya ukimya, Baba Mtakatifu ametembelea Ukuta wa kifo, mahali pa mateso na mauaji ya kinazi. Baba Mtakatifu pia ametembelea chumba cha njaa na mahali alipofungwa na hatimaye kuuwawa kikatili Mtakatifu Marximilliano Maria Kolbe, takribani miaka 75 iliyopita.

Baba Mtakatifu ametembelea pia kambi ya Birkenau, umbali wa kilometa tatu kutoka kambi ya Auschwitz. Ni mahali ambapo maiti ya waliouwawa kikatili ilikuwa ikichomwa moto. Hapa wafungwa walihukumia kifo cha taratibu. Mwishoni Baba Mtakatifu katika hali ya ukimya na majonzi makuu alitembelea mnara wa kumbu kumbu ya kimataifa uliojengwa kunako mwaka 1967, mahali ambapo kunaonesha kilio cha watu waliokata tamaa, mahali ambapo zaidi ya watu millioni 1. 5 waliuwawa kikatili, lakini wengi wao ni Wayahudi kutoka katika sehemu mbali mbali za Bara la Ulaya. Auschwitz- Birkenau: 1940 – 1945.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.