2016-07-23 17:28:00

Mbinu mkakati wa kudumisha ukuu na utakatifu wa ndoa!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM katika mkutano wake mkuu wa 17 huko Luanda, Angola kuanzia tarehe 18 – 25 Julai 2016 ambao unaongozwa na kauli mbiu “Familia Barani Afrika: Jana, Leo na Kesho kadiri ya mwanga wa Injili imekuwa ni fursa makini kwa familia ya Mungu Barani Afrika kuweza kujiwekea mikakati madhubuti ili kukabiliana na changamoto zinazoendelea kuibuliwa na ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia dhidi ya Injili ya familia.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican Askofu Salutaris Melchior Libena wa Jimbo Katoliki Ifakara, Tanzania anazungumzia baadhi ya mambo yaliyogusiwa na Mababa wa SECAM katika mkutano wao huko Luanda, Angola, wakati huu tunaposubiri ujumbe kwa familia ya Mungu kutoka SECAM. Anasema, Mababa wa SECAM wamejadili kwa kina na mapana mchango wa vyombo vya habari pamoja na athari zake katika mafungamano ya maisha ya ndoa na familia.

Wamegusia mazingira na sababu mbali mbali zinazopelekea wanandoa kutengana au kuachana na matokeo yake na utume wa familia kutekelezwa na mzazi mmoja ambaye mara nyingi ni mwanamke. Hali hii inapelekea malezi tenge. Mababa wa SECAM ili kuimarisha utume wa familia Barani Afrika kwa namna ya pekee wamekazia maandalizi ya kina kuhusu mafundisho ya Kanisa juu ya ndoa na familia inayoundwa kati ya bwana na bibi wanaopendana kwa dhati kwa lengo la kushiriki katika kazi ya uumbaji pamoja na kutambua kwamba, watoto ni zawadi kutoka kwa Mungu.

Wanandoa watarajiwa watambue haki, wajibu na dhamana yao katika kutangaza, kukuza, kudumisha na kushuhudia Injili ya familia Barani Afrika. Kuna haja pia ya kuwaelimisha vijana kutambua maana ya ndoa ya Kikristo ili wasaidie pia kuwainjilisha vijana wenzao. Wakleri waandaliwe vyema tangu wakiwa Seminarini ili waweze kusaidia kukuza na kudumisha utume wa familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.