2016-07-15 14:05:00

Papa alaani vikali mauaji ya kigaidi huko Nice, Ufaransa


Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa masikitiko makubwa mauaji ya kigaidi dhidi ya watu 84 yaliyotokea mjini Nice, Alhamisi tarehe 14 Julai 2016 wakati Ufaransa ilipokuwa ikiadhimisha Siku kuu ya kitaifa. Baba Mtakatifu katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin Katibu mkuu wa Vatican anasema, kwa mara nyingine tena Ufaransa imekumbukwa na kutikiswa na mashambulizi ya kigaidi yaliyopelekea watu wengi wakiwepo watoto kupoteza maisha.

Baba Mtakatifu analaani kwa nguvu zote vitendo vyote vya kigaidi na anapenda kuonesha uwepo wake wa karibu kwa njia ya kiroho na wanachi wote wa Ufaransa lakini kwa namna ya pekee anapenda kuwaweka watu wote waliofariki dunia kwenye shambulizi hili chini ya huruma ya Mungu. Baba Mtakatifu anawaombea majeruhi wote ili waweze kupona haraka na kuendelea na shughuli zao za kila siku. Baba Mtakatifu anapenda pia kuchukua nafasi hii kuombea amani na maridhiano nchini Ufaransa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.