2016-05-23 15:36:00

Papa Francisko akutana na Imam Mkuu Al Tayyib wa Chuo Kikuu cha al Azhar


Baba Mtakatifu Francisko Jumatatu hii majira ya adhuhuri, akiwa katika makazi yake ya kitume Vatican, alitembelewa na Imam Ahmad Muhammad Al-Tayyib,  Mkuu wa Chuo cha Al Azhar cha Misri, ambacho mafundisho yake ya Kiislamu, yana mamlaka makubwa ya kiteolojia  kwa Waislamu Washiite.

Kwa mujibu wa Ofisi ya habari ya Vatican, kati ya walioambatana na Imam Mkuu Profesa Al-Tayyib,  ni pamoja na Prof. Abbas Shouman ambaye ni  Katibu Mwandamizi katika Chuo cha  Al-Azhar;  Profesa  Mahmaoud Hamdi Zakzouk, Mjumbe katika Baraza la ngazi ya juu la Wasomi katika Chuo Kikuu cha  Al-Azhar, pia alikuwepo Mkurugenzi wa Kituo cha Al-Azhar  ajili ya mazungumzo. Wengine ni Mwanasheria  Mohamed Mahmoud Abdel Salam,Mkurugenzi na  Imamu;  Prof. Mohie Afifi Afifi Ahmed, Katibu Mkuu katika kitengo cha Utafiti kwenye masuala ya Kiislamu; Balozi Mahmoud Abdel Gawad, Mshauri wa Imam Mkuu Tayyeb kwa  masuala ya Kidiplomasia;  Tamer Tawfik, Mkurugenzi; na Ahmad Alshourbagy pamoja na  Balozi Hatem Seif Elnasr wa Jamhuri ya Kiarabu ya  Misri katika  Jimbo Takatifu.

Imam Mkuu Al-Tayyib, alipokewa  Vatican na Kardinali Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya mazungumzo na dini zingine, ambaye aliandamana na ugeni huu hadi walipokutana na Papa , upande wa Vatican alikuwepo pia  Katibu wa Idara ya Vatican, inayohusika na mambo ya nchi za nje Msgr. Miguel Ángel Ayuso Guixot.

Habari inasema, mazungumzo ya Papa na mgeni wake , yaliyodumu kwa muda wa nusu saa, yalifanyika katika hali urafiki mkubwa , ambamo kati ya mengine wamegusia uwepo wa majadiliano kati ya Kanisa Katoliki na Uislamu. Na kisha dhamira ya pamoja juu ya mamlaka na waamini wa dini kubwa  duniani, dhamira ya kukataa  vurugu na ugaidi, hali ya Wakristo katika mazingira ya migogoro na mivutano ya  kisiasa na kijamii katika Mashariki ya Kati na ulinzi kwa jumuiya ndogo ya Wakristo. Mwishoni mwa maongezi yao, Papa alitoa kwa Imam Mkuu Tayyib, zawadi ya medali ya Mzeituni kama ishara ya amani na nakala ya waraka wake wa kuitunza Dunia kama nyumbani kwa wote  maarufu kwa jina la "Laudato Si".

Baada ya kukutana na Papa , Imam Mkuu al Tayyib, pia alifanya mazungumzo mafupi na Kardinali Tauran, kabla ya  hajaondoka katika  jengo la Kitume,  la Vatican. Mwezi Februari mwaka huu, Msgr. Miguel Angel Ayuso Guixot, alikwenda  Cairo Misri, kupeleka barua ya  Kardinali Jean-Louis Tauran, ambayo ilitoa mwaliko kwa Imamu Mkuu Tayyib kukutana na Papa Francisko mjini Vatican. 








All the contents on this site are copyrighted ©.