2016-04-09 12:18:00

Sadaka kwa maskini ni kielelezo cha huruma!


Jumamosi majira ya asubuhi katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Baba Mtakatifu Francisko alitoa Katekesi yake kwa mahujaji na wageni kama sehemu ya mwendelezo wa maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu. Mafundisho ya Papa yalilenga katika  Injili ya Matayo 6,1-4, somo lenye kuhimiza utoaji wa sadaka bila kujionyesha au kutafuta makuu. Papa alionya  Mungu hatoi thawabu kwa sadaka zinazotolewa kwa nia za kujionyesha.  Na alisisitiza utoaji wa sadaka lazima uwe  kisiri siri , kimyakimya tena kwa unyenyekevu na  bila mbwembwe, kiasi kwamba hata mkono wa kushoto usijue kiinachotolewa na  mkono wa kulia. ”Sadaka na itolewe kwa siri ,na Baba aonaye sirini atajaza kilichopungua”.

Papa aliendelea kufafanua juu ya Somo hilo, akisema  huongoza katika  kugundua kipengele muhimu katika  matendo ya huruma na  utoaji wa sadaka. Na alionya kwamba,  inaweza onekama kama ni jambo jepesi  kutoa sadaka, lakini si hivyo kwa kuwa tunatakiwa kuwa waangalifu, ili sadaka tutoayo isionekana kama tendo la majivuno au kutaka kujionyesha mbele ya wengine au kama tu wema sana. Maelezo ya Papa yalirejea  neno hili  sadaka  katika asili yake ya Kigriki akisema, ina maana  ya huruma.  Kwa hiyo,  kwa maneno mengine,  sadaka ni huruma.  Na kwamba, huruma huweza onekana kupitia mambo na mifano mingi, inayolenga kupunguza  makali  ya upungufu kwa wahitaji.

Na kwamba , utoaji wa sadaka si jambo geni lakini limekuwepo nyakati zote tangu wakati wa Agano la Kale, imeandikwa jinsi  Mungu,  alivyotoa angalisho maalum kwa maskini  wasiokuwa na kitu, wageni, yatima na wajane. Pamoja na kukumbusha  wajibu huo, pia  Mungu anataja kama jambo muhimu kwamba , sadaka ni lazima itolewa  kwa  ukarimu  kama zawadi,  bila  ya moyo  kuhuzunika. (Kumb 15:10). Hii ikiwa na maana kwamba, sadaka ni  upendo , upendo wenye kufurahia na kuona fahari  katika kusaidia wengine wahitaji .  Ni kutoa  kwa  sababu umeguswa na mahangaiko ya wengine bila ya kuona kama ni  mzigo au kutaka kuondokana na kero  ya muombaji kwa haraka iwezekanavyo. Papa alieleza na kukikumbuka  kisa cha Nabii Tobias , ambaye  baada ya kupokea kiasi kikubwa cha fedha, alimwita mwanawe na kumpa maneno ya hekima akisema :kwa wale wote wote wanaotenda haki hutoa sadaka. Na usimpe kisogo maskini yoyote , na hivyo Mungu pia hatakupa kisogo Tb 4,7-8).  Papa ameyataja maneno haya kuwa ni maneno ya busara sana  yanayoweza kutusaidia kuelewa thamani ya kutoa sadaka.

Na  alirejea  mafundisho ya Yesu aliyowachia wafuasi wake, ambamo akataza kutoa sadaka kwa kujionyesha na mbwembwe.Sadaka isitolewa kwa nia za kujitafutia sifa kwa watu  lakini katika kutambua kwamba kuna watu waliopungukiwa na mahitaji muhimu. Na upande mwigine, haipaswi kuonekana kama ni kosa kwa mtu anayeomba msaada . Na hivyo  kumbe ni muhimu kutoa sadaka  tukiwa na utambuzi kwamba , kuna watu wanaohitaji msaada wa haraka,   bila kutazama  nani  anaomba au hadhi ya mtu anayeomba.  Aidha Papa ametoa wito wa kutofautisha kati ya maskini na aina mbalimbali za ukosefu wa huduma unaowafanya watu kuwa maskini.  Papa alieleza na kusema  kwa kifupi sadaka ni  tendo la upendo  kwa mtu anayeomba ambaye tunakutana nae. Na tunapaswa kutoa msaada huo bila mtu mwingine kujua tulichotoa.   

Papa alieleza na kutoa mwaliko  wa kuyafanya maneno ya Mtume Paulo kuwa maneno yetu : Ni heri kutoa kuliko kupokea " (Matendo 20:35; taz 2Kor 9,7).








All the contents on this site are copyrighted ©.