2016-03-21 14:41:00

Kardinali Pietro Parolin ziarani Bulgaria


Katibu wa Jimbo la Papa, Kardinali Pietro Parolin,  mapema Jumapili  iliyopita  aliwasili nchini Bulgaria, ambako  aliongoza liturujia ya  kutabaruku  Kanisa Kuu  la Bikira Maria Mpalizwa Mbinguni, ambalo ni Sehemu ya Makao Makuu ya Kitume nchini  Bulgaria. Katika homilia yake, Kardinali aliutumia muda huo kufikisha salaam za upendo kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, ambaye kwa moyo mkuu hufuatilia maisha ya Jumuiya ya Wakatoliki nchini Bulgaria, ambayo  ingawa ni ndogo, lakini ni hai. 

Kwenye tukio hili, Kardinali Parolin, amehimiza Wakatoliki wa Bulgaria kuendelea kuiweka hai roho ya Watakatifu Cyril na Methodi,  pamoja na kudumisha udugu na Waotodosi  na wito wa kukaribisha waamini wa imani nyingine  hata wale wasiokuwa na uhusiano nao wowote wa kidini.  Aliwakumbusha umuhimu wa kufanya hivyo  hasa katika Mwaka huu wa huruma, na hasa  umuhimu kujali  kuhudumia maskini wa maskini na walio katika mateso na wanyonge. Aidha Kardinali  alikumbuka kwamba katika kanisa hilo  pia alitolea sala zake kwa mara ya kwanza, mjumbe wa Kitume wa  kwanza  nchini  Bulgaria,  Askofu Mkuu Angelo Roncalli ambaye baadaye alichaguliwa kuwa Papa na kuchagua jina la  Papa Yohane XXIII - na pia amemtaja Papa Yohane Paulo II, aliyesisita  umuhimu wa kudumisha maisha ya mashahidi Bulgaria, Askofu Yevgeny Bosilkov na Mapadre watatu wa Shirika la  Bikira Maria Mpalizwa Mbinguni ”Assumptionists” waliopigwa  risasi wakati wa Ukomunisti.

Katibu wa Jimbo la Papa, Kardinali Pietro Parolin, mwishoni mwa hotuba yake ya kutabaruku hilo   Kanisa Kuu,  alilikabidhi chini ya usimamizi  na ulinzi wa Bikira Maria Mpalizwa Mbinguni..

 Kanisa hilo lililojengwa katika miaka ya 1924, ambalo limefanyiwa ukarabati , lilikuwa halijawahi wekwa wakfu ila kubarikiwa tu.  Hivyo  Jumapili iliyopita Kardinali  Kardinali Parolin, aliliweka Wakfu katika Ibada ya Misa aliyoiongoza akisaidiana na Mjumbe wa Kitume wa Papa , Askofu Mkuu  Anselmo Guido Pecorari, pia Rais wa  Baraza la Maaskofu Katoliki  Bulgarian, Askofu Mkuu  Christo Proykov, na Maaskofu wengine wawili Katoliki. Katika Ibada hii alikuwepo pia Askofu Mkuu wa Antonio wa Kanisa la Kiotodosi, Msimamizi wa Kanisa hilo katika eneo la Ulaya Magharibi.  Miongoni mwa wawakilishi wa serikali, alikuwepo Rais wa Bunge la Bulgaria Tsetska Tsatcheva, Makamu wa Rais wa Jamhuri, Margarita Popova, na Naibu Waziri Mkuu Premier, Meglena Kuneva. 








All the contents on this site are copyrighted ©.