2016-03-21 06:55:00

Ajali ya ndege yasababisha vifo vya watu 62


Baba Mtakatifu Francisko amesikitishwa na vifo vya watu 62 vilivyotokea mwishoni mwa juma huko Russia baada ya ndege ya abiria kuanguka. Baba Mtakatifu katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, anawaombea marehemu wote hawa raha na mwanga wa milele ili uweze kuwaangazia na kupumzika kwa amani. Baba Mtakatifu anapenda kuwafariji wale wote walioguswa na msiba huu mzito ili Mwenyezi Mungu aweze kuwapatia nguvu, awafariji na kuwapatia matumaini.

Wachunguzi wa mambo wanasema, pengine ajali hii imesababishwa na hali mbaya ya hewa iliyokuwa inaambatana na upepo mkali uliosababisha rubani wa ndege hii kushindwa kuona vyema wakati ikiwa katika taratibu za kutua uwanja wa ndege wa Rostov, huko Russia. Ndege ya Shirika la Ndege la FlyDubai ilikuwa inatoka Dubai, Falme za Kiarabu ikiwa na abiria 55 na wafanyakazi wa ndege 7.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.