2016-03-09 11:29:00

Tanzania na Uingereza kuendelea kushirikiana katika masuala ya kiuchumi!


Tanzania na Uingereza zinatarajia kuendelelea kushirikiana katika masuala ya Uchumi kupitia Mpango wa Ushirikiano wa Kiuchumi kati ya Tanzania na Uingereza “UK partnership in Prosperity” ambao unajikita katika maeneo makubwa ya ushirikiano ya Mafuta na Gesi, Nishati Jadidifu; Kilimo; na Uboreshaji Mazingira ya Biashara. Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama ambaye alimwakilisha Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kufanya mazungumzo na Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika, Mhe. James Duddrige, terehe 08 Machi, 2016, Jijini Dar es Salaam.

Tunatarajia mpango huu ukishafanyiwa maboresho utaimarisha uchumi wa nchi zote mbili, tunatarajia baada ya maboresho hayo makampuni mengi kutoka uingereza kuja kufanya biashara nchini kuwekeza .Tunaelewa nia ya serikali ya Uingereza kuwekeza  katika miundo mbinu iliyopo vijijini hasa katika sekta ya maji na kilimo hii itasaidia kuinua maisha ya wananchi wanaoishi vijijini hasa wanawake , hii ni kutokana na kuwa asilimia 80 ya wananchi nchini wanaishi vijijini na wengi wao ni wananawake na leo ukizingatia ni siku ya wanawake Duniani” Alisema Mhagama.

Aliongeza kuwa mpango huo umekuja muda muafaka wakati serikali inaendelea na juhudi za kuishirikisha sekta binafsi katika kukuza uchumi nchini kwa kuwa serikali inatambua sekta binafsi ndio chachu ya maendeleo nchini.

“Tunahitaji ushirikiano wenu ili muweze kutujengea uwezo wa kuwavutia wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kwa msingi wa kuendeleza viwanda nchini na hatimaye tunaweza kufanya kwa ubora  biashara kimataifa ” alisistiza. Waziri wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Afrika, Mhe. James Duddrige ali fika ofisini hapo kwa lengo la kuonana na Waziri Mkuu kwa ajili ya kumueleza ushirikiano wao watakaoendelea kuutoa kwa serikali ya awamu ya tano katika masuala ya Dawa za kulevya na biashara haramu ya pembe za ndovu nchini pamoja na uboreshaji wa Mpango wa Ushirikiano wa Kiuchumi kati ya Tanzania na Uingereza “UK partnership in Prosperity”  . Mpango huo wa Ushirikiano wa Ushirikiano Kati ya Tanzania na Uingereza ulizinduliwa rasmi Novemba 2015 na Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda.

 

Imetolewa na

KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI

OFISI YA WAZIRI MKUU 








All the contents on this site are copyrighted ©.