2016-03-07 07:58:00

Ikiwa kama kasi ya ukataji wa miti itaendelea hivi! Tanzania kugeuka jangwa!


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira nchini Tanzania Bw. Luhaga Mpina amesema mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa nane hapa nchini ambayo inakabiliwa na tishio la kugeuka jangwa kutokana na tatizo la ukataji miti hovyo. Aliitaja mikoa hiyo kuwa ni Simiyu, Mwanza, Mara, Singida na Arusha. Mingine ni Kilimanjaro, Dodoma na Manyara.

Ametoa kauli hiyo hivi karibuni alipopewa nafasi na waziri Mkuu Kassim Majaliwa awasalimie wananchi waliofika kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi kwenye jengo la utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Busega mkoani Simiyu. Alisema kila wilaya imepewa agizo la kupanda miche milioni 1.5 kwa mwaka na kwa sababu hiyo watawapima wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na wakurudenzi wa halmashauri na Manispaa ambao hawatafikisha idadi hiyo ya miche na kuwasilisha majina yao kwa Waziri Mkuu.

"Ilani ya Chama cha Mapinduzi imeagiza kila wilaya ipade miche milioni 1.5 kwa mwaka. Kwa hiyo kuanzia Machi 3, mwaka ambayo ni siku ya upandaji miti, tutawamoniter Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wote ili kubaini ni nani hajatekeleza agizo hili. Tutakuletea mezani kwako majina ya wale ambao watashindwa kutekeleza agizo hili ambalo liko kwenye Ilana ya CCM," alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri huyo alisema amekuja na miche 7,000 ya matunda aina ya miembe, michungwa na mifenesi ambayo ameahidi kuigawa kwa kila wilaya. "Tunataka katika ziara yako hii tusambaze miche 5,000 kwa kila jimbo la mkoa huu na wakati unamaliza ziara yako tutakuwa tumesambaza miche 35,000," alisema. Naibu waziri Mpina alisema kupandwa kwa miti mbalimbali ya matunda, kutawasaidia wananchi kupata matunda ya kula, ya kuuza na kupata fedha lakini pia itawasaidia kuwa chanzo cha mali ghafi kwenye viwanda vya kusindika matunda.

Imetolewa na Ofisi ya Waziri mkuu wa Tanzania.

 








All the contents on this site are copyrighted ©.