2016-01-25 08:37:00

Dhamira ya Kristo na Kanisa ni kutangaza Habari Njema kwa Maskini


Jumapili, katika  hotuba yake fupi  kabla ya sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtaktifu Francisko, alitafakari Injili ya Siku iliyoeleza jinsi Yesu alivyohubiri katiika Sinagogi la mji wake Nazareti, akirejea  aya kutoka Kitabu cha Nabii  Isaya: "Roho wa Bwana yu juu yangu, kwani amenitia mafuta,  kuleta habari njema kwa maskini. Papa Francisko alifafanua kwamba, Yesu mwenyewe alitimiza unabii wa Isaya, kama ilivyosikika katika somo la Injili . 

Alisema, hiyo ndiyo  dhamira ya Yesu, na utume wa Kanisa,  kuhubiri habari njema kwa maskini. Na kwamba, ingawa Habari Njema   inahubiriwa  kwa  watu wote , Papa alielezea, Yesu  anatoa kipaumbele zaidi kwa wale waliombali nae, walio katika  mateso, wagonjwa na walio telekezwa na jamii kutokana na hali yao duni kimaisha. Aliwataja  Maskini,  hasa ndio  walengwa katika  Injili.

Baba Mtakatifu Francisko aliendelea  kueleza nini maana ya kutangaza kwa  maskini habari njema. Alisema zaidi ya yote, ina maana kuwa karibu na maskini, kuwatumikia kwa furaha , kuwapa  habari ya kukomboa dhidi ya ukandamizaji.  Yote hayo, yakifanyika  katika jina  na Roho wa Kristo, kwa sababu Yesu  ndiye  Injili ya Mungu mwenyewe, Yeye ni Huruma ya Mungu, Yeye ni ukombozi wa Mungu. Baba Mtakatifu alieleza na kuhoji iwapo  kazi za uinjilishaji katika parokia hutoa kipaumbele  kwa maskini  zaidi katika Parokia, na iwapo hiyo ndiyo azma kuu kwa vyama na jumuiya za Kanisa. Na  iwapo  waamini ni aminifu katika mpango huo wa Kristo?

Aliweka bayana kwamba , kupeleka habari njema kwa maskiini haina maana tu kutoa msaada wa kijamii au  kisiasa,  lakini inahusu kutenda kwa nguvu ya Injili ya Mungu, yenye kuleta wongofu mioyoni , kuponya waliojeruhiwa na   kufanya mageuzi  mazuri katika uhusiano wa kijamii kwa mujibu wa mantiki ya upendo

Baba Mtakatifu alikamilisha hotuba yake kwa kuomba msaada wa Mama Bikira Maria, Mama wa Waenezaji Injili,  awasaidie wote kupata hamu na kiu ya kutaka kueneza Injili duniani kote, na hasa kuifikisha Injili katika mioyo ya maskini wengi wa kiroho , na kumwezesha kila  mmoja na kila muumini na jumuiya nzima ya kikristo,  kuwa shahidi imara wa huruma ya Mungu, ambayo hutoka kwa Kristo. 








All the contents on this site are copyrighted ©.