2016-01-13 15:55:00

Tanzania kuendeleza ushirikiano na Qatar pamoja na Kuwait


Waziri mkuu wa Tanzania, Kassim S. Majaliwa amekuatana na kufanya mazungumzo na mabalozi wawili kutoka nchi za Qatar na Kuwait.  Akizungumza kwa nyakati tofauti na mabalozi hao siku ya Jumatano, tarehe 13 Januari 2016, ofisini kwake, Magogoni jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu amewashukuru mabalozi hao kwa pongezi walizokuja kumpatia, pamoja na namna ambavyo nchi zao zimekua zikisaidia Tanzania, ambapo ameahidi kuendeleza ushirikiano mzuri baina ya Tanzania na nchi zao.

Kwa upande wake, Balozi wa Qatar, Abdallah Jassim al Maadad amesema Serikali yake itaendelea kuisaidia Tanzania katika maeneo yote ambayo Qatar imepiga hatua kubwa na inaweza kutoa msaada kwa Tanzania. Amesema Quwait iko tayari kuwekeza nchini katika sekta ya kilimo, kwa vile ardhi ya Tanzania ni yenye rutuba na inafaa kwa shughuli za kilimo. Aidha, ametaja sekta nyingine ambazo wangependa kuwekeza ni pamoja na sekta ya uvuvi na viwanda.

Naye, Balozi wa Kuwait, Jasem Al Najem ambaye amekuja kujitambulisha kwa Waziri Mkuu, amesema nchi yake kupitia ‘Kuwait fund’ iko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania katika miradi mbalimbali ya maendeleo. Balozi Najem, pia ameshauri vituo vya uwekezaji vya Tanzania na Kuwait kufanya kazi kwa ushirikiano zaidi ili kurahisisha utekelezaji wa miradi mbalimbali.

Na mwandishi maalum.








All the contents on this site are copyrighted ©.