2016-01-12 09:49:00

Serikali ya Tanzania inafanya utafiti ili kutoa ada elekezi kwa shule binafsi!


Wakati wa kampeni za kugombea Urais nchini Tanzania kwenye Uchaguzi mkuu wa Mwaka 2015 kati ya hoja zilizokuwa na nguvu na mashiko, ilikuwa ni elimu ya bure kwa watanzania kuanzia shule za awali hadi shule za Sekondari kwa Chama cha Mapinduzi! UKAWA ikasema, ingetoa elimu ya bure kwa watanzania kuanzia shule ya awali hadi Chuo kikuu! Watanzania wakajiuliza maswali ya msingi, Je, fedha itapatikana wapi? Dr. Magufuli ameonesha kwamba, ikiwa kama Watanzania watajikita katika nidhamu, maadili, sheria na kanuni za kazi kuna uwezekano mkubwa wa kufanya maboresho kwa maisha ya watanzania wengi. Hapa siri ya urembo ni kujituma, uaminifu, tija na weledi kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi!

Watanzania wanaanza kufaidi elimu bure kufuatia kufunguliwa kwa shule za umma huku Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, akisema fedha zimeshafika kwa kila shule. Aidha, Prof. Ndalichako amewataka wamiliki wa shule binafsi kujitathmini. Itakumbukwa kuwa serikali ilipoanzisha Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi na Sekondari mwaka 2000, lengo lilikuwa ni kutoa ruzuku ya Sh.10,000 kwa kila mwanafunzi wa shule ya msingi na Sh. 25,000 kwa kila mwanafunzi wa shule ya sekondari kwa mwaka. Ruzuku hiyo inalenga kugharimia ununuzi wa vitabu vya kiada na ziada, vifaa vya kufundishia zikiwamo chaki, madaftari, kalamu za risasi na wino, karatasi za kufanyia mitihani, ukarabati miundombinu ya shule na shughui za utawala.

Hivi karibuni Prof. Ndalichako alisema kuwa fedha za ruzuku kwa wanafunzi shule za msingi na sekondari, zimeshapelekwa, lengo likiwa ni kuhakikisha leo wanafunzi wanaanza masomo. “Fedha hizi zitakuwa zikitolewa kwa awamu, kwa hiyo zilizokwenda ni awamu ya kwanza tu,” Alisema Profesa Ndalichako. Prof. Ndalichako alisema ili kuhakikisha fedha zote zinazotolewa zinafika kwa walengwa, watashirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), kuhakikisha zinawafikia walengwa.  Alisema moja ya njia ya kufikia lengo hilo ni kutoa fedha hizo kwa awamu na kuhimiza uaminifu kwa watu wote wanaohusika.

Ada Elekezi Kwa Shule Binafsi: Akizungumzia ada elekezi, alisema suala hilo ameona ni vyema lifanyiwe utafiti kwa kila shule kufafanua matumizi ya fedha wanazotoza na kuwa baada ya kukubaliana ada elekezi, watakaokiuka watakabidhiwa kwa Mamlaka ya Mapato (TRA), ili watozwe kodi.  “Hili suala nimelikuta na nikaona ni vyema tufanye utafiti kidogo. Sasa hivi shule nyingi tayari zina viwango vya ada na vina tofauti kubwa tu. Kwa kuanzia, nimeona tuanze na ada zilizopo, tayari nimeshaelekeza na kazi imeanza kwa kutaka wamiliki wa shule watoe `justification’ (hoja za kuhalalisha) ada wanazotoza,” alisema na kuongeza:

“Nimeona kuna umuhimu wa kushirikisha hawa watu na kuwasikiliza, ndiyo maana tukasema kwanza wao watupatie hayo maelezo. Mtu aseme labda anatoza Sh. milioni tano, atuambie ana walimu wangapi, mishahara yao Sh. ngapi? Gharama za umeme ni Sh. ngapi?  "Akisema gharama za chakula na sisi tunazijua, tutaangalia hata kama anawapa watoto soseji, tutaangalia bei na kadhalika, tunachotaka kwanza tutafute uhalisia wa hizo ada.

“Najua kuna baadhi ya maeneo tutakosa uhalisia maana mwingine anatoza bei ya umeme labda kila mwanafunzi Sh. 20,000, kama ana wanafunzi 500, jumla yake itakuwa Sh. ngapi? Tutamwambia atupe bili ya umeme tuthibitishe,” alisema Pro. Ndalichako. Alisema wameamua kufanya hivyo kwa kuwa shule binafsi zina mazingira tofauti na hivyo ni vigumu kuwa na ada elekezi moja ambayo kweli inatekelezeka. “Ada elezi haiwezi kuwa sawa kwa sababu shule zina viwango tofauti na walimu aina tofauti. Hata maeneo zilipo, ni tofauti, pia kuna huduma tofauti zinazotolewa na shule hizi. Kila shule ikitoa mchanganuo, tujua kilichopo, tukiwa na data (takwimu) itatusaidia kujua mengi na sisi kujipanga vizuri, hata vyakula wanavyotoa tutaviangalia na kuvihakiki, usije kutoza Sh.15,000 kwa chakula kwa siku halafu ukampa mtoto ugali na maharage,” alisema.

Alisema pamoja na mambo mengine, vitu hivyo vitathibitishwa na wakaguzi wa shule na pale inapobidi wazazi watashirikishwa ili kupata uhalisia. “Tutachukua muda, lakini tutakuja na majibu ambayo Watanzania wote watakubali kwa sababu sasa hivi wapo ambao hawapo na sisi wizara, hatutaki kumwambia mtu anayetoa kompyuta, na vitu vingine muhimu kwa mwanafunzi aache. "Lazima tushirikiane nao ili hata kwenye utekelezaji tufanikiwe, ambacho hatutaki ni shule kutumia sana wanafunzi kama sehemu ya kipato na tukiweka ada elekezi wale watakaotoza zaidi, tutawapeleka TRA wawatoze kodi kwa sababu hawa wanafanya biashara, wanazalisha,” alisema Prof. Ndalichako.

Na mwandishi maalum.








All the contents on this site are copyrighted ©.