2015-12-02 07:42:00

Afrika iwe ni mfano bora wa kumwilisha Jubilei ya huruma ya Mungu!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anasema, Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kitume Barani Afrika amejisikia nyumbani na Waafrika wamemwonjesha, upendo, ukarimu na heshima kubwa kwa kuwajali na kuwathamini. Jamhuri ya watu wa Afrika ya Kati kilikuwa ni kiini cha safari hii ya kitume Barani Afrika, ili kuwatia shime ili waweze kuvuka kutoka katika hali yao ya sasa tayari kuanza ukurasa mpya wa maisha.

Baba Mtakatifu alipenda kwenda Afrika ambako kunaonekana na wengi kuwa ni pembezoni mwa jamii, ili kuihamasisha Familia ya Mungu Barani Afrika kusimama kidete kupambana na umaskini, ujinga na maradhi daima wakiambata utu na heshima ya binadamu, msingi wa maendeleo kwa siku za usoni. Baba Mtakatifu alipokuwa anazungumza na kundi la vijana; wakleri na watawa alikuwa anaweka pembeni hotuba aliyokuwa ameandaa ili kuwashirikisha watu hawa kile kilichokuwa kimefichika katika sakafu ya moyo wake.

Baba Mtakatifu Francisko ni mtu wa majadiliano, haya yamejionesha kwa kuwahusisha waamini kwa kuitikia au kwa njia ya maswali, si mtu anayependa sana hotuba zilizoandikwa, zinamnyima ile raha ya kuzungumza na kuwasikiliza watu! Baba Mtakatifu aliwashangaza wengi alipoanza kuchukua dondoo za kufanyia kazi, wengi wakabaki wamepigwa na butwaa! Vijana walijisikia vizuri kabisa kwa uwepo wa Baba Mtakatifu miongoni mwao, wengi walionesha uso wa tabasamu, meno njeeee!.

Padre Lombardi anaendelea kufafanua kwamba, uzinduzi wa maadhimishi ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei kuu ya huruma ya Mungu ni kati ya matukio yatakayobakiza chapa ya kudumu katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Amefungua lango la Jubilei ya huruma ya Mungu Jimbo kuu la Bangui, mwaliko kwa waamini kukimbilia ili kuambata huruma, upendo, msamaha, haki na upatanisho unaobubujika kutoka katika undani wa maisha yao. Kwa kitendo hiki, Bangui unakuwa ni mji mkuu wa maisha ya kiroho, huko kwenye shida na magumu, kwenye changamoto na kinzani za maisha, ndiko Kanisa linakotumwa kwenda kutangaza huruma ya Mungu.

Padre Lombardi anakaza kusema, tukio hili ni utangulizi wa pekee katika uzinduzi rasmi wa maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei kuu ya huruma ya Mungu, utakaofanyika hapo tarehe 8 Desemba 2015 kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na baadaye sehemu mbali mbali za dunia. Hii ina maana kwamba, huruma ya Mungu inapatikana mahali popote pale, jambo la msingi ni waamini kuwa tayari kuiambata huruma hii katika maisha yao.

Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kufungua maadhimisho ya Jubilei kuu ya huruma ya Mungu alipata nafasi ya kushiriki katika mkesha wa sala pamoja na vijana. Aliwaungamisha vijana watano na baadaye makundi makubwa ya vijana yaliweza kuungama usiku ule! Si rahisi katika mazingira ya Bangui kuonana na makundi makubwa ya vijana yakijisadaka kutoka nje ili kwenda kushiriki katika tukio hili. Baba Mtakatifu aliwaonjesha ule ujasiri na jeuri ya imani, ili kutoka kifua mbele, tayari kushuhudia imani inayojikita katika matendo.

Mwaka wa Jubilei kuu ya huruma ya Mungu ni mwaliko kwa waamini kukimbilia huruma ya Mungu katika maisha yao kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho. Familia ya Mungu Afrika ya Kati, imeonesha jinsi ya kuadhimisha Mwaka Mtakatifu wa Jubilei kuu ya huruma ya Mungu, yaani kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani!

Padre Lombardi anasema kati ya changamoto kubwa zilizokuwa mbele ya Baba Mtakatifu Francisko ni kuhusu usalama, amani na utulivu kwa watu waliokuwa wanakusanyika kwa ajili ya maadhimisho mbali mbali, lakini Baba Mtakatifu ameonesha ujasiri wa imani na matumaini ya kutaka kuwaimarisha ndugu zake katika imani, matumaini, haki, amani na upatanisho, tayari kuanza ukurasa mpya wa maisha. Huu ni mwendelezo wa ujasiri ambao pia umekwisha oneshwa na Mtakatifu Yohane Paulo II alipotembelea Sarayevo wakati mtutu wa bunduki unarindima na Papa mstaafu Benedikto XVI alipotembelea Lebanoni wakati hali ya usalama ikiwa tete! Mapapa wanakwenda mahali ambapo kuna shida, ili kuwatia shime watu wasikate tamaa, bali wawe na ujasiri wa kusonga mbele kwa kumtumainia Mwenyezi Mungu.

Padre Lombardi anasisitiza kwamba, kabla ya kuondoka kwenda Jamhuri ya Afrika ya Kati kuna kiongozi wa ngazi ya juu kabisa alishauri kwamba, isingekuwa busara kwa Baba Mtakatifu kutembelea Msikiti mkubwa wa Bangui ili kukutana na waamini wa dini ya Kiislam, lakini baada ya Baba Mtakatifu Francisko kutembelea, kusali na kuzungumza na waamini wa dini ya Kiislam kwenye Msikiti huo kwa furaha na uwazi, alipigwa na bumbuwazi na kumwambia Padre Lombardi kwamba, kweli Baba Mtakatifu ni moto wa kuotea mbali! Amethubutu kwenda kule ambako wengi waliohofia, matendo makuu ya Mungu na jambo hili limewagusa waamini wengi waliokutana na kumwona Baba Mtakatifu akiwa msikitini mwao, cheche ya kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini.

Padre Lombardi akigusia kuhusu ugonjwa wa Ukimwi anasema, Kanisa Barani Afrika limekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi. Baba Mtakatifu katika majibu yake kwa waandishi wa habari alipokuwa anarejea kutoka Afrika amelizungumzia suala la ugonjwa wa Ukimwi katika mapana kwamba, linapaswa kushughulikiwa mintarafu: haki, amani na maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili; kwa kupambana na umaskini, ujinga na maradhi. Kanisa linaendelea kukazia umuhimu wa kuzingatia kanuni maadili na utu wema; kwa kujizuia na kuwa waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa.

Wagonjwa wa Ukimwi wapatiwe dawa za kurefusha maisha na wanawake wajawazito wakingwe ili wasiwaambukize watoto wao virusi vya Ukimwi wanapozaliwa! Baba Mtakatifu amekazia umuhimu wa Amri za Mungu kama dira na mwongozo wa maisha adili. Mwenyeheri Anuarite Nengapeta ni shuhuda wa uaminifu katika usafi wa moyo, mfano bora wa kuigwa na waamini wengine. Ni Mtawa alijejisadaka kwa ajili ya huduma kwa maskini akasimama kidete kutetea usafi wa moyo dhidi ya wale waliokuwa wanawaka tamaa ya mwili!

Baba Mtakatifu Francisko Barani Afrika amejionea mwenyewe umati wa vijana wa kizazi kipya wakiwa na nyuso za furaha na matumaini ya kesho iliyo bora zaidi. Watoto na vijana ni jeuri ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake kwa sasa na kwa siku zijazo. Hiki ni kielelezo cha imani na matumaini ya Kanisa; kundi linalopaswa kuwezeshwa ili kushiriki vyema katika mchakato wa maendeleo ya Bara la Afrika. Kanisa linaendelea kukua na kukita mizizi yake katika maisha ya watu; lina matatizo, changamoto na mafanikio yake. Kanisa linapaswa kuwa ni kwa ajili ya watu pamoja na watu katika uhalisia wa maisha yao, ili kujenga na kuimarisha majadiliano ya kidini na kiekumene; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na maridhiano.

Padre Lombardi anasema, Baba Mtakatifu Francisko akiwa Bangui, alizunguka uwanjani akiwa amekaa na Imam, ujumbe makini kabisa kwamba, waamini wa dini hizi mbili wanaweza kuishi kwa pamoja na kushikamana kwa ajili ya ustawi na maendeleo yao na kwamba, tofauti zao za kidini ni utajiri mkubwa. Kanisa kwa kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema ili kudumisha majadiliano, amani, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.