2015-11-04 15:24:00

Papa atafakari faida za kuomba msamaha na kuheshimiana ndani ya familia


Baba Mtakatifu anasema,  kama ndani ya familia, tutajifunza kuomba samahani  na kuheshimiana mmoja kwa mwingine, kuifunga siku kwa kuomba msamaha bila kuchelewa,  tutaweza jenga  familia thabiti zaidi na hata kupunguza ukatili ndani ya jamii.

Papa ametoa rai hiyo wakati wa Katekesi yake kwa mahujaji na wageni kama mwendelezo wa majadiliano , kufuatia kukamilika kwa Sinodi ya Maaskofu iliyotafakari umuhimu wa Familia katika  utume wa kanisa na jamii kwa ujumla.  Hata hivyo alionya kwamba maelezo yake si kwamba yanatoa maamuzi yake ya  mwisho juu ya majadiliano ya Sinodi ya familia, bado muda wa kufanya hivyo , maana  anahitaji muda zaidi ya kutafakari yaliyojadiliwa. Lakini  bado ni muhimu kuzungumzia mada hii ya familia, kutokana na umuhimu wake  kwamba, ndani yake kuna kujifunza mengi , kama pia  shule ya kwanza, ya kujifunza  maisha na thamani ya kuomba  msamaha.  Maelezo ya Papa yalilenga katika maneno ya  sala ya Baba yetu, ambamo waamini kila siku  huomba kusamehewa kwa yale waliyokosea na pia huomba  neema ya kusamehe wengine.

Papa alionyesha kutambua jinsi ilivyo vigumu kusamehe , lakini akasema ni hitaji muhimu katika ukomavu wa mtu binafsi na katika uwezo wa kutambua  na kukiri makosa yetu na kufanya marekebisho katika  mahusiano yaliyo vunjika au kulegalega. Tendo la kuomba msamaha, huanzia  ndani ya  familia. Na kwamba msamaha ni kiungo chenye kuongeza upendo ulio imara zaidi kati ya wanafamilia,  katika kutembea pamoja kwenye njia yao ya maisha. Na  hufanya jamii kwa ujumla, kuwa na  upendo zaidi na ubinadamu zaidi. Papa anaitaja familia  kuwa ni jiwe kuu la msingi katika kujenga maisha yetu na ishara fasaha katika  utambulisho wa kuwa mfuasi wa  Kikristo na katika kutii mapenzi ya Baba wa Mbunguni .

Papa aliendelea kusema, ni lazima kuwa na utambuzi kwamba , maisha hayasimami na hasa maisha ya familia yanaendelea kusonga mbele, kamwe hayasimami. Hvyo familia daima ziko safarini , zikiendelea kuandika kurasa na kurasa za uzuri wa maisha ya kiinjili kwa familia.  Na hasa katika dunia ambayo wakati mwingine inakuwa na ukame wa maisha na upendo , inapaswa kila siku kuzungumzia juu ya zawadi hii kubwa ya ndoa na familia.

Katika mafundisho  haya , Papa amesisitiza msamaha , kusamehe na kuheshimiana mmoja kwa mwingine, kuwa ni nguzo kuu ya maisha yenye ya furaha , yenye kuwa na  upendo wa dhati, kama zawadi ya thamani yenye kuidumisha familia, kwa  majitoleo ya sadaka binafsi  kwa ajili ya wengine.  Amesema bila uwepo wa  kusamehe, na  bila upendo,  familia kama hiyo husambaratika mara.  Papa alieleza na kurejea mara kwa mara juu ya sala ya Baba  Yetu, iliyofundishwa na Yesu mwenyewe. “Utusamehe  makosa  yetu,  kama nasi tunavyowasamehe waliotukosea, na pia  Yesu alisema: "Mkiwasamehe watu wengine makosa yao, Baba yenu aliye mbinguni  pia atawasamehe ninyi (Mathayo 6,12.14-15).   Na hivyo , Papa akaonya , haiwezekani  kuishi bila kusamehe, na hasa  uwepo wa maisha mazuri ndani ya familia, kwa kuzingatia kwamba, makosa  kwa mara nyingi  hutokana na  udhaifu wetu wa kibinadamu, ikihamasishwa na ubinafsi wetu. Na hivyo kumbe  kile kinachohitajika  kwa kila mmoja, ni kuona umuhimu wa kuponya majeraha  yanayoumiza.  Haifai kuuguza kidonda kwa muda mrefu bila kukipatia dawa, maana kwa kadri kinavyokaa bila dawa ndivyo huzidi kuchimbika. Kumbe ni kufanya hima kuponya madonda  hayo.  Ni hitaji la kuomba msamaha  na kuomba  mapatano iwe kati ya  mume na mke, au kati ya wazazi na watoto,, au kaka na dada,  mkwe na mama mkwe  n.k . 

Baba Mtakatifu akitoa Katekesi hii kwa lugha ya Kiitalino alionyesha imani yake kwamba,  familia zina uwezo wa kutembea pamoja katika njia  ya Heri  zilizo fundishwa na Yesu.  Kujifunza na kufundisha jinsi ya kuomba msamaha  au kusamehe mara moja, kwa  kuheshimiana,  kwa ajili ya uponyaji wa majeraha  yanayoweza kujitokeza katika safari ya  ndoa  na familia. Na hivyo  msamaha na kuheshimiana vinakuwa  shina  imara  la maisha  mazuri yaliyo imara zaidi  yenye kupokelewa kama zawadi kati ya wanafamilia.  Papa alieleza huku akionyesha imani yake kwamba, kwa hakika familia za Kikristo leo hii , zinaweza fanya mengi  na pia kwa ajili ya Kanisa.   Kwa maoni hayo, Papa alionyesha hamu yake kwamba katika Jubilee ya Huruma ya mungu , familia zitaweza gundua upya nguvu za msamaha, na  kuiwezesha familia kubwa ya Kanisa kutangaza nguvu za upatanisho na  upendo wa Mungu, ili pasiwe na mtu anayesahaulika katika msamaha huu  katika maisha yetu ya kila siku.








All the contents on this site are copyrighted ©.