Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameteuliwa kuwa Mjumbe wa Tume ya Kimataifa ya Kuchunguza Jinsi ya Kugharimia Elimu Duniani – The International Commission on Financing Global Education Opportunity. Tume hiyo, inayoongozwa na Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Mheshimiwa Gordon Brown ambaye pia ni Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa (UN) wa Elimu Duniani ina jumla ya wajumbe 30, wakiwemo marais na mawaziri wakuu wa zamani, wataalam wa elimu, wafanyabiashara kutoka sekta binafsi na wawakilishi wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali (NGO’s) duniani.
Tume hiyo imeteuliwa na viongozi watano duniani wakishirikiana na Katibu Mkuu
wa Umoja wa Mataifa na ilitambulishwa kwa mara ya kwanza katika mkutano uliofanyika
Septemba 29, mwaka huu, 2015 mjini New York, Marekani. Rais Kikwete alihudhuria mkutano
huo wa kwanza wakati wa ziara hiyo Marekani ambako pia alikuwa anaongoza Jopo ya Watu
Mashuhuri Duniani ambao wanaangalia jinsi dunia inavyoweza kujiandaa vizuri zaidi
dhidi ya magonjwa ya milipuko.
Viongozi walioteua Tume hiyo ni Mheshimiwa Erna Solberg ambaye ni Waziri Mkuu wa Norway,
Mheshimiwa Michelle Bachelet Rais wa Chile, Mheshimiwa Irina Bokova ambaye ni Mkurugenzi
Mkuu wa UNESCO, Mheshimiwa Peter Mutharika Rais wa Malawi na Mheshimiwa Joko Widodo
Rais wa Indonesia. Tume hiyo ya Elimu itawasiliana
na kukutana na viongozi mbali mbali duniani, wabuni sera za elimu na watafiti wa masuala
ya elimu ili kuiwezesha Tume hiyo kujenga hoja zinazokidhi umuhimu wa kuwepo kwa upatikanaji
wa fedha za kutosha na uwekezaji katika kuleta usawa katika upatikanaji wa nafasi
za elimu kwa watoto wa kike na kiume.
Aidha, Tume hiyo italenga kuangalia jinsi gani dunia inavyoweza kuongeza uwekezaji katika elimu katika muda mfupi na katika muda mrefu na itapendekeza aina ya uwekezaji na hatua za kuchukuliwa. Pia, Tume hiyo itapendekeza njia za kuwashawishi wakuu wa nchi na Serikali, mawaziri wa fedha, uchumi, elimu na ajira, magavana wa majimbo na serikali za mitaa pamoja na viongozi wa kibiashara na wawekezaji kuchukua hatua za kuwezesha ongezeko kubwa la fedha katika sekta ya elimu.
Miongoni mwa watu ambao watatumikia kwenye Tume hiyo pamoja na Rais Kikwete ni
Rais wa zamani wa Mexico Mheshimiwa Felipe Calderon, Rais wa zamani wa Kamisheni ya
Ulaya Mheshimiwa Jose Manuel Barroso, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Dangote Group Bwana
Aliko Dangote, Waziri Mkuu wa zamani wa Australia Mheshimiwa Julia Gillard, Rais wa
Benki ya Dunia Mheshimiwa Jim Kim, na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Alibaba Group ya
China, Bwana Jack Ma.
Wengine ni Mama Graca Machel wa Msumbiji, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Econet Wireless
Group ya Zimbabwe Bwana Strive Masiyiwa, Mwanamuziki Shakira Mebarak, Waziri wa zamani
wa fedha wa Marekani na Rais wa Heshima wa Chuo Kikuu cha Harvard Bwana Lawrence Summers
na Bi. Helle Thorning Schmitt, waziri mkuu wa zamani wa Denmark.
Na mwandishi maalum.
All the contents on this site are copyrighted ©. |