2015-06-20 08:33:00

Dr. Ali Mohamed Shein atangaza nia ya kuwania Urais Zanzibar


Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar, ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein hivi karibuni amechukua fomu ya kuomba ridhaa ya kuwania nafasi ya Urais wa Zanzibar na kueleza matumaini yake ya kuendelea kuchaguliwa kutokana kuwa na sifa zote za kuwa Rais wa Zanzibar.

Dk. Shein alichukua fomu hiyo katika Ofisi Kuu ya CCM Zanzibar iliopo Kisiwandui mjini Unguja majira ya asubuhi akikabidhiwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai akiwa ni mwana CCM pekee kuchukua fomu katika ngazi hiyo tokea kuanza mchakato.

Viongozi mbali mbali walimshindikiza Dk. Shein akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Idd pamoja na mkewe Mama Mwanamwema Shein na viongozi wengine mbali mbali ambapo mara baada ya kuchukua fomu alipata fursa ya kuzungumza na wana CCM na wananchi waliofika katika hafla hiyo.

Katika maelezo yake Dk. Shein alitoa shukrani kwa wanaCCM waliojitokeza kwa wingi katika hafla hiyo kwa lengo la kuimarisha chama hicho huku akieleza sababu kubwa zilizomfanya kuchukua fomu hiyo ikiwa ni pamoja na kuendeleza hatua za maendeleo yaliofikiwa pamoja na kuendeleza wimbi la ushindi wa chama hicho kama ilivyo kawaida katika kila uchaguzi mkuu.

Dk. Shein alisema kuwa anaamini ataendelea kuungwa mkono na wananchi walio wengi pamoja na kuwa na sifa, uwezo, uzoefu wa kutosha katika chama na utendaji wa kazi katika Serikali zote mbili ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa CCM Zanzibar kwa uwamuzi wao wa kimaendeleo wa kuendeleza harakati za Mapinduzi kwani yote hayo ni kwa ajili ya maendeleo ya Zanzibar huku akitoa shukurani kwa wanaCCM na wananchi kwa kuendelea kumuunga mkono kwa kumchagua mwaka 2010 sambamba na kuendelea kuwa na matumaini ya kumchagua tena mwaka huu.

Dk. Shein alisema kuwa katika kipindi chote alichoingia madarakani mafanikio makubwa yameweza kupatikana ikiwa ni pamoja na kutekeleza Ilani ya CCM, ambayo hadi hii leo tayari imeshatekelezwa kwa asilimia 90 na kuwa na matumaini ya kufikia asilimia 100 baada ya miezi minne yapo. Aidha, Dk. Shein alishangazwa na baadhi ya viongozi kujipa sifa na kujisifu ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kueleza kuwa yote yanayofanywa ndani ya Serikali hiyo huamuliwa na Baraza la Mapinduzi ambalo huwahusisha viongozi wote Serikali.

Alisema kuwa iwapo CCM itampitisha kuwa mgombea wa Urais kwa tiketi ya chama hicho aliahidi kuendelea kufanya kazi katika wazifa huo kwa ufanisi mkubwa bila ya woga wala hofu huku akisisitiza jambo la msingi ni kuyalinda na kuyaendeleza Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 sambamba na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Dk. Shein pia alitumia fursa hiyo kuwaeleza wananchi na wanaCCM pamoja na wapenda amani wote kuwa atawashughulikia kwa mujibu wa Katiba na Sheria za nchi wale wote watakaotaka kuvuruga amani na utulivu uliopo. Alisisitiza kuwa hatochelea kumchukulia hatua yeyote atakaevuruga amani huku akieleza azma ya kuendelea kusimamia uchumi ambao umeendelea kukua kwa kiasi kikubwa katika uongozi wake.

Aidha, alieleza kuwa ataendelea kuutetea Muungano wa Serikali mbili na kuahidi kuudumisha kwani ndio Sera za CCM . Pia alieleza azma yake ya kuendelea kusimamia Utawala Bora, kuendeleza mchakato wa uchimbaji gesi na mafuta hapa Zanzibar sambamba na kufanya kazi kwa uwazi na uwajibikaji.

Alisema kuwa wakati anaingia madarakani uchumi ulikuwa umekwua kwa asilimia 5.2 lakini katika uongozi wake hadi hivi leo uchumi umeendelea kukua kwa asilimia 7.2 hukua akieleza kuwa kwa mwezi kulikuwa kunakusanywa Tsh.Bilioni 13.5 wakati hivi sasa kwa mwezi kunakushanywa Tsh. Bilioni 39 sambamba na kukua kwa pato la mtu mmoja mmoja.

Dk. Shein alisema kuwa ataendelea kuisimamia misingi ya uchumi imara ili izidi kuimarika ikiwa ni pamoja na kukamilika kwa ujenzi wa uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume mnamo mwezi wa Oktoba mwaka huu sambamba na uwekaji wa taa katika uwanja wa ndege wa Pemba kazi ambayo inaendelea pamoja na azma ya kuujenga majengo ya kisasa katika uwanja huo.

Pia, Dk. Shein alieleza kuwa azma ya kujengwa Bandari mpya ya Mpigaduri ipo na hivi sasa imefikia hatua nzuri kwani azma hiyo ilianza katika Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Dk. Salmin Amour Juma katika mpango wa kuwa na Bandari Huru na sio kama inavyozungumzwa na watu wengine.

Alisema kuwa hivi sasa tayari mradi huo umeshakubaliwa na michoro, ramani na fedha tayari zimeshatafutwa. Katika mazungumzo kati yake na waandishi wa Habari Dk. Shein aliwaeleza mipango ya Zanzibar ya kuwa na miji minne ya kisasa, kuendelezwa kwa Maeneo Huru ya Vitegauchumi, kuongeza kasi ya utendaji kazi, kuendeleza michezo pamoja na miundombinu yake, kuliimrisha Shirika la Meli, Bandari, ununuzi wa meli nyengine ya mafuta na mambo mengineyo.

Nao viongozi wa CCM wakitoa shukurani na pongezi zao kwa Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar walieleza kuwa Rais Bora anatoka CCM na sio katika chama chengine chochote cha upinzani na Dk. Shein ndio wanaemtarajia kuwa Rais wa Zanzibar.

Na mwandishi maalum.








All the contents on this site are copyrighted ©.