2015-05-16 12:50:00

Papa : jengeni moyo wa majadiliano katika jamii


Ijumaa  15 Mei 2015, Baba Mtakatifu Francisko alikutana na Maaskofu Katoliki toka Jamhuri ya Kati(CAR) , kama sehemu ya ziara yao ya kitume katika Kiti Kitakatifu. Katika hotuba yake kwa Maaskofu hao, alisisitiza  kuboresha mazungumzo baina ya dini na imani mbalimbali, kama njia ya kujenga mapatano, ushirikiano na kusameheana kwa upendo,  kwa  jamii yao, iliyotumbukizwa katika dimbwi la chuki na vurugu. 

  Papa alitoa wito huo kwa Maaskofu wa CAR, kama jibu kwa maelezo ya Maaskofu wa CAR,  juu ya hali halisi za maisha ya Kanisa na kijamii katika taifa la Afrika Kati ambalo kwa kipindi cha karibia miaka miwili, limeishi katika vurugu mbaya za kivita kati ya Waislamu na makundi ya Kikristo  yaliyoasi na kuchukua silaha kupambana na Waislamu. Vurugu zilizo sababisha maelfu ya watu kuuawa na  Mamilioni wengine, kulazimika kuhama makazi yao.

Baba Mtakatifu katika hotuba yake kwa Maaskofu kwa moyo wa kibaba na udugu, alionyesha kujali mateso makubwa ya watu wa CAR, yanayotokana na  utengano wa kidini na kimadhehebu.Na alishukuru pia kwa juhudi zinazofanywa na Kanisa Katoliki, hasa katika kusaidia waathirika wa unyanyasaji na wale waliokimbia  makazi yao bila ubaguzi .  Alionyesha kutambua ugumu wa kazi za kitume na kichungaji kwa wakati huu. Lakini akasisitiza kwamba,  wakati chuki na vurugu  vinapopamba moto , ni wakati kwa  Wakristo, kutoa jibu la kwa upole,  msamaha na upendo wa Kiinjili.  Papa alionyesha kujuta kwamba, bahati mbaya , jibu hilo bado halijapata nafasi kwa mioyo mingi ya Wakristo, wanapopambana na ukatili na matatizo ya nyakati , kama ilivyotokea huko CAR. Hivyo hii inakuwa ni ishara wazi kwamba ,Injili bado kujipenyeza kwa dhati ndani ya  mioyo ya watu kila mahali, kuwashawishi  mabadiliko huru chanya katika tabia za Wakristo.

Pamoja na hili, Papa pia aliwahimiza Maaskofu kutokatishwa tamaa na migogoro  hiyo lakini waendelee kupata mbadala katika njia ya imani na matumaini, kuleta  upya hisia za msisimko na mabadiliko, kupitia kazi zao za uinjilishaji. Na kwamba wao kama Maaskofu  wanao wajibu usiokwepeka  katika utoaji wa shuhuda za kinabii, katika utendaji wa kimaadili , kama msingi wa muhimu wa haki, ukweli na  uaminifu msingi wa mchakato wowote upya. Katika hali hii, pia  aliwasihi waendelee na Juhudi zao, kuboresha mazungumzo na amani, kupitia ukuzaji wa ushirikiano kati ya waamini wa dini mbalimbali na makabila, akisema  kufanya hivyo kutasaidia kuhamasisha maridhiano na mshikamano wa kijamii.

Pia Papa aligeukia  suala la malezi ya Kikuhani, akisema kuna haja  kutoa msisitizo juu maana ya ubinadamu na upendo wa Kristo katika malezi Waseminaristi,  kwa ajili ya kujenga ufahamu wa kutosha juu ya maisha aminifu katika viapo vya useja, kwa kuwa hakuna makubaliano mengine yanayoweza kukubalika kwa maisha ya Kipadre. Papa alihitimisha hotuba yake, na maneno ya kutia moyo na msaada kwa ajili ya familia, akisema , familia isisahaulike katika juhudi zao ziote kwa kuwa familia ni nafasi nzuri ya kujifunza, na kutenda  mazoezi utamaduni wote wa maisha ya kusamehe, amani na maridhiano, vipengere vinavyohitajika sana katika taifa la Jamhuri ya Afrika Kati.

 








All the contents on this site are copyrighted ©.