2015-05-11 09:46:00

Yesu anatupenda hata kama hatustahili


Jumapili wakati wa sala ya malaika wa Bwana ,  Papa akisalimia mahujaji  na wageni waliokusanyika katika uwanja wa kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, alitafakari somo la Injili ya Yohana, Sura ya 15, ambamo Yesu anatoa amri mpya  kwa wanafunzi wake , wapendane  kama  yeye alivyowapenda , “Pendaneni kama mimi nilivyowapenda ninyi".

Baba Mtakatifu alisema, maneno hayo ya Yesu, yanatoa ujumbe mzima wa maisha ya Yesu hapa duniani kwamba, Mungu alimpenda binadamu hata akamtoa mwanae pekee sadaka, ili binadamu apate tena stahili ya kuitwa Mwana wa Mungu. Ni kuwa na upendo wa  sadaka ya maisha kwa ajili ya wengine. Yesu alisema "Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu: kuyatoa maisha yake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru.  Yesu aliwaambia wanafunzi wake wakati wa Karamu ya mwisho, katika Chumba cha juu.  Huo ni muhtasari wa yote yaliyofanywa na  Yesu, kuutota sadaka uhai wake kwa ajili ya rafiki zake, tena marafiki ambao walikuwa bado hawajaelewa kina cha upendo wake,  wa kuwa  tayari  kutelekezwa, kusalitiwa na kukataliwa.  Hili linatuambia sisi pia kwamba, Yesu  anatupenda, hata kama hatustahili  upendo wake.  Yesu alitupenda hivyo!

Baba Mtakatifu aliendelea  kusema , kwa njia hii, Yesu anatuonyesha njia ya kufuata,  njia ya upendo.  Na kwamba,  amri yake  si amri nyepesi , inayoweza kuchukuliwa kama kitu cha ziada au  kuwa nje ya heshima na maisha. Lakini daima ni amri msingi ya kufuatwa katika maisha. Na ni amri mpya ya Kristo, kwa kuwa Kristo alikuwa wa kwanza kuifanikisha , kuutoa mwili na uhai wake kwa sababu ya binadamu mwingine na mara kuandikwa  katika moyo wa mwanadamu (taz Yer 31:33), tena kwa  moto wa Roho Mtakatifu.

Kwa maelezo hayo, Papa alitoa wito kwa waamini wote, kutembea katika njia hii ya upendo, akisema , ni njia halisi, inayowataka waamini kuupeleka upendo huu kwa  wengine. Ni kupeleka upendo wa Mungu  kwa jirani. Ni wote kutembea pamoja. Na kwa namna gani tunaweza kuwa na uhakika tunatembea katika njia  kamili ya upendo huu, Papa Francisko ametoa mfano ni katika kuwajali watoto na watu wazima, wenye   elimu na  wasiokuwa na elimu, matajiri na maskini, watu wema na wenye dhambi, wote ni kuwakaribisha katika moyo wa Kristo. Wote ni kujazwa na  upendo  wa kukomboa, ni kuwekwa  huru kutoka ubinafsi.  

Papa aliendelea kusema,  Upendo huu huchota nguvu zake kutoka Ubatizo. Na kwa neema ya Mungu na imani ya Kanisa, mbatizwa hupadikizwa  katika shina la mzabibu wa kweli, ambaye  ndiye Kristo. Ni kupita kutoka katika kifo hadi maisha, na kuwezeshwa kurejea kwa Mungu kama Baba .  Papa anasema kuna mambo mengi madogo na makubwa  ya kutenda katika kutii amri ya Bwana: "Pendaneni kama nilivyowapenda ninyi".  Papa ametaja kati ya ishara ndogondogo  katika maisha ya kila siku ni huduma kwa wazee,  watoto, mgonjwa, mtu mpweke na mwenye  mashaka, watu wasio na makazi, ajira, wahamiaji, wakimbizi ... Papa alieleza na kutoa shukurani za dhati kwa nguvu ya Neno la Kristo, ambalo humwezesha kila anayeliamini , kujenga moyo wa upendo na fadhila, kwa  wake kwa waume upendo wanaokubali mafundisho ya Kristo.

Baada ya hotuba yake, Papa alisalimia makundi mbalimbali, na kwa namna ya pekee alitoa salaam zake kwa kundi kubwa la watu walioshiriki katika  Matembezi  kwa ajili ya  Maisha. Alisema ni muhimu kufanya kazi kwa pamoja kwa ajili ya  kutetea na Kukuza Maisha. Miongoni wa kundi hilo, alikuwa ni Kardinali Raymond Burke.  Pia Papa alitoa salaam zake kwa adhimisho la Siku ya Mama Dunian. Papa aliwatakia Mama wote , tunaoishi nao na hata wale wanaoishi nasi kiroho, Baraka za Bwana na kuwaweka chini ya usimamizi wa Mama Maria, Mama wa Yesu. Na  kuwaomba wote wasisahau kumwombea. 








All the contents on this site are copyrighted ©.