2015-04-27 14:20:00

WAZIRI CHIZA: changamkieni fursa za uwekezaji Visiwani Comoro!


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Mhe. Mhandisi Christopher Chiza aliwaeleza baadhi ya wafanyabiashara kutoka Tanzania, kuchangamkia fursa za biashara na uwekezaji visiwani humo wakati alipotembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Comoro akiwa na baadhi ya wafanyabiashara Ijumaa tarehe 24 Aprili, 2015 kuonana na Balozi wa Tanzania Visiwani Comoro Bw. Chabaka Kilumanga na kupata maelezo juu ya kazi zinazofanywa na Ubalozi huo Visiwani humo.

Akizungumza na wafanyabiashara Ubalozini hapo Waziri Chiza aliwaeleza kuwa, zipo fursa nyingi ambazo wanaweza kuzitumia kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania katika visiwa hivyo na kuangalia namna ya kutumia nafasi hiyo.“Zipo nafasi nyingi za kibiashara na uwekezaji, kinachotupasa watanzania ni kuwa na nia ya dhati na mwamko wa kwenda kuangalia nafasi za biashara kwa nchi za wenzetu japo zipo changamoto kama za usafirishaji wa bidhaa kwenda visiwani Comoro lakini tukijipanga vema tutaweza kuzikabili changamoto hizo ambapo tutaweza kujenga mahusiano makubwa na mazuri ya kibiashara kati kati ya nchi hizi mbili” alisisitiza Mhe. Chiza.

Akizungumza na wafabyabiashara hao, balozi wa Tanzania Visiwani Comoro Bw. Chabaka Kilumanga alieleza kuwa, Ubalozi wake umejipanga kutangaza nafasi za uwekezaji na shughuli ambazo Tanzania inaweza kuzifanya nchini Comoro ili kuweza kupanua wigo wa uwekezaji na kujitangaza zaidi Visiwani humo. “ipo haja ya kufanya maonesho ya bidhaa za Tanzania nje ya nchi kama hatua moja wapo ya kukuza soko la bidhaa za Tanzania na hii itasaidia kuonesha ni nini Tanzania na Comoro inaweza kufanya kwa pamoja ili kuweza kukuza uchumi kwa nchi hizi mbili”,alisema.Bw. Chilumanga alieleza kuwa, Ubalozi wa Tanzania Visiwani Comoro unategemea kuanzisha Tume ya Pamoja ya ushirikiano kati ya Tanzania na Comoro utakaosaidia kurahisha masuala ya Uwekezaji na Biashara, na shughuli zingine za kibalozi visiwani humo.  

Imetolewa na Francisca Swai

Afisa Habari, Kitengo cha Mawasiliano

Ofisi ya Waziri Mkuu - Comoro








All the contents on this site are copyrighted ©.