2015-04-18 15:02:00

Tanzia: Kardinali Francis E. George wa Chicago amefariki dunia


Vatican inaendelea na maombolezo ya kuondokewa na watumishi wake katika  Dekania ya Makardinali, kufutia kifo kingine  kilichotokea Ijumaa usiku tarehe  17 April 2015, cha Kardinali Francis E. George, OMI, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la  Chicago, Marekani. Marehemu aliyestaafu mwaka jana 2014, pia aliwahi kuwa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki  Marekani  (USCCB) kati ya mwaka 2007-2010. Kardinali George, amefariki  akiwa na umri wa miaka 78, baada ya kusumbuliwa na maradhi ya kansa kwa muda mrefu .

Baba Mtakatifu Francisko, baada ya kupoeka taarifa hizi, amepeleka salaam zake za rambi rambi kwa njia ya telegram iliyotiwa sahihi na Katibu wa Jimbo la Papa,Kardinali Pietro Parolin, kwa Askofu Mkuu Blase Cupich wa Jimbo Kuu la Chicago, ambamo ameonyesha kusitikishwa na taarifa hizo . Papa ametoa rambirambi hizi kwa Mapadre , watawa na waamini wote wa Jimbo Kuu la Chicago, na pia kwa mwakilishi wake nchi Marekani,Askofu Mkuu Carlo Maria Viganò.

Papa ameyakumbuka maisha na utumishi wa Marehemu na kutoa shukrani kwa ushuhuda ulioonyeshwa na  Kardinali George katika maisha ya  kujitenga kama  mwanashirika wa Oblate ya Mary Immaculate, na  kwa utumishi wake katika utume wa  elimu, na  huduma yake ya  kiaskofu katika Makanisa ya Yakima, Portland na Chicago. Kwa moyo wa majonzi, amesema, anaungana na wote katika sala za kuiombea roho ya Mtumishi huyo aliyekuwa amejaliwa hekima,busara na unyenyekevu wa kichungaji, kupokelewa katika  upendo na huruma ya Mungu Baba yetu wa mbinguni. Aidha Papa amefariji wote  wanaoombeleza msiba huu, na tumaini  la uhakika la ufufuo, na  kuwaomba wapokee  Baraka zake za upendo wa Kitume kama amana ya faraja na amani katika Bwana.
 

 Askofu Mkuu Kurtz wa Jimbo la Luisville Kentucky , ambaye pia ni Rais wa USCCB,  akitangaza kifo cha Kardinali George, anasema , kifo cha mtumishi huyu wa kanisa, kinatia simanzi zaidi, hasa wakati huu wa furaha ya ufufuko wa Bwana. Na kwamba  alikuwa ni mtumishi mwema wa kanisa, mfano wa kuigwa na wengi . Na pamoja na kuhuzunika lakini pia wanapata kuwa na  amani ya moyo  katika utambuzi kwamba,  baada ya mateso mengi,  sasa ameikamilisha safari yake katika mkono wa Bwana . Uongozi wake hautasahaulika  akiwa  Askofu Mkuu wa Chicago na Rais wa USCCB,  ambamo aliwaongoza kwa ukarimu na unyenyekevu mkubwa , akihimiza kila mmoja kuona jinsi Mungu  ambavyo hutufanya wote kuwa familia moja,  kaka na  dada,  mmoja na mwingine.

Askofu Kurtz, akiwa ameungana na  ndugu zake katika uaskofu, kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi ya maisha ya  ushuhuda ya Kardinali George, na amewaalika waamini wote kumkumbuka katika sala zao,  kuombea  nafsi yake ipate pumziko la amani.








All the contents on this site are copyrighted ©.