Baba Mtakatifu katika Katekesi yake kwa mahujaji na wageni, ameonyesha kujali kwamba, bado juhudi zaidi zinahitajika, kwa ajili ya kufanikisha usawa na uelewa kamili juu ya tofauti za kijinsia kati ya mwanamke na mwanamme katika maisha ya kijamii na kikanisa pia . Sauti ya wanawake ni lazima isikilizwe na maoni yake kupewa uzito hasa wakati wa maamuzi. Papa alitoa msisitozo huo , mapema Jumatano hii, akiendelea na katekesi yake juu ya mada ya familia, sehemu ya kumi, ambamo ameangalia zaidi kiini cha familia ambacho ni Mme na Mke. Amesema ni zawadi kubwa ya Mungu kwa wanadamu, kwa kumuumba kwa mwanamume na mwanamke na kuwaunganisha pamoja katika sakramenti ya ndoa. Papa alitazama kwa makini zaidi juu ya tofauti za kimaumbile kati ya mwanamume na mwanamke, katika kilele cha uumbaji wa Mtakatifu wa Mungu.
Mafundisho ya Papa, yamenukuu zaidi Maandiko Matakatifu ya Biblia juu ya uumbaji , kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Mwanzo, akisema, tunasoma kwamba Mungu, baada ya kuumba ulimwengu na viumbe vyote, aliikamilisha kazi yake ya uumbaji kwa kumuumba binadamu kwa mfano wake mwenyewe: "kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba" (Mwanzo 1: , 27),ndivyo kinavyosema kitabu cha Mwanzo.
Papa aliendelea kuzungumzia tofauti za kijinsia zilizoko katika mfumo wa Maisha, lakini akisisitiza kwamba , wote wawili, mwanamume na mwanamke, hubeba ndani yao sura na mfano wa Mungu, kama maandiko Matakatifu ya Biblia yalivyorudia kutaja mara tatu katika mistari miwili (26-27). Mwanamume na mwanamke ni sura na mfano wa Mungu. Hii inatuambia kwamba si tu mwanaume aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu, na wala si tu mwanamke aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, lakini ni wote wawili mwanamume na mwanamke, kama wanandoa, wao ni mfano wa Mungu. Na tofauti ya maumbile kati ya mwanaume na mwanamke si kwa ajili ya upinzani, au mmoja kuwa chini ya mwingine , lakini kwa ajili ya ushirika na mwendelezo wa kizazi, daima wote wawili wanaendelea kuwa katika sura na mfano wa Mungu.
Papa anasema, uzoefu unatufundisha kujua vizuri zaidi na kukua katika ushirikiano
wa binadamu kwa ajili ya kukamilishana katika mahitaji ya maisha yenye usawa kati
ya mwanaume na mwanamke. Kumbe hakuna madhara kati ya tofauti hizi za kimwili. Wote
wawili wameumbwa kwa ajili ya kusikilizana na kusaidiana. Papa ameeleza na kuasa kwamba,
bila kuwa na utajiri wa kuheshimiana , iwe katika mawazo , au katika mahusiano,
upendo na kazi, pia katika imani , wote wawili hawawezi kuelewa kwa kina nini maana
ya kuwa mwanaume na mwanamke.
Papa aliendelea kutazamisha katika utamaduni wa kisasa, ambao umefungua nafasi mpya
, uhuru mpya na kina kipya kwa ajili ya utajiri wa ufahamu katika utofauti huu.
Lakini pia umezua pia mashaka mengi na ubabe mwingi. Papa kwa mshangao alitoa mfano
wa nadharia zinazotafuta uwepo wa tofauti hizi katika haja za kujamiiana katika ngono
eti tu kwa sababu wao hawawezi tena kukabiliana nayo. Amelitaja hili ni tatizo kubwa
linalohitaji kujadiliwa zaidi, ili kujua zaidi kwa kina juu ya upendo wa kweli kati
ya mwanaume na mwanamke katika maisha ya ndoa. Iwapo kuna kasoro ni lazima kutibu
kwa heshima na kushirikiana na urafiki. Papa anasema pamoja na mapungufu haya ya
kibinadamu, kwa mkono na neema ya Mungu, inawezekana kuwa na muungano ndoa na familia
kwa ajili ya maisha. Dhamana ya ndoa na familia ni jambo zito na muhimu kwa kila
mtu, si tu kwa Waumini. Papa alihimiza wasomi kutoiweka pembeni mada hii, kama vile
ni si jambo la msingi katika utendaji wa jamii iliyo huru zaidi na haki zaidi.
Papa alikamilisha mafundisho yake kwa kutazama wajibu wa Kanisa katika hili akisema,
huu ni wajibu mkubwa wa Kanisa, waamini wote, na hasa familia za waamini, zinapaswa
daima kugundua upya, uzuri wa ubunifu wa Muumbaji katika kuwaumbe mke na mme kwa
mfano wa Mungu. Na ndivyo mwanamume na mwanamke hutafutana kati yao pamoja na
Mungu.
Papa ametaja changamoto iliyoko mbele ya Kanisa na waamini na familia leo hii hasa ni katika kungundua uzuri wa mpango wa Mungu, katika utumilifu wa kazi yake ya kuumbua mtu kwa sura na mfano wake. .
All the contents on this site are copyrighted ©. |