2015-03-17 15:14:00

Barua ya Papa Francisko kwa Maaskofu katoliki Nigeria


Baba Mtakatifu Francisko, katika kipindi hiki cha Kwaresima, amewaandikia barua ndugu zake  Maaskofu Katoliki wa Nigeria, ambamo ameomba pia wafikishe salaam zake kwa Jumuiya za Kikristo walizopewa  dhamana  katika huduma za kichungaji, akionesha  mshikamano  na mawazo yake kwa  hali ngumu na changamoto wanazokabiliana nazo kwa sasa.

Katika barua hiyo, Papa amesema, “wakati huu tunapotembea kuelekea ufufuko wa Yesu Kristo tukiwa tumeungana pamoja na Kanisa  zima, ninapenda kutoa saalam zangu za dhati , kwenu nyote Maaskofu Wakuu na Maaskofu wa Nigeria na pia naomba mzifikishe kwa  jamii Kikristo mliyokabidhiwa katika huduma ya kichungaji.  Aidha ninapenda kushirikishana nanyi, baadhi ya mawazo  yangu kuhusu hali halisi za sasa  za maisha  katika nchi yenu”.

Barua ya Papa, imeendelea kuitaja nchi ya Nigeria, taifa kubwa kuliko yote Barani Afrika, yenye kuwa na raia zaidi ya milioni 160, yenye kujulikana kama kinara si Barani Afrika tu lakini  duniani kote.

Papa ametaja kwa jinsi taifa hilo katika miaka ya hivi karibuni  limeweza kushuhudia ukuaji wa haraka wa uchumi  na pia kwa mara nyingine kujiwasilisha katika jukwaa la kimataifa kama soko la kuvutia, kutokana na  uwepo wa rasilimali, na kwa uwezo wake wa kibiashara. Na pia kwa jinsi linavyojitambulisha lenyewe kuwa mtendaji mkuu katika utatuzi wa migogoro  ya kisiasa Barani Afrika.

Lakini wakati huohuo, taifa lao linakabiliwa na matatizo makubwa, ikiwa ni pamoja na aina mpya ya vurugu za kuvuka mipaka na misimamo mkali inayoendeshwa kwa misingi ya  kikabila, kijamii na kidini, ambamo kwayo Wanigeria wengi wameuawa, kujeruhiwa na kuwa vilema; kutekwa na kupokonywa  kila kitu si mali tu lakini hata na wapendwa  wao,  nchi yao, maisha yao, utu wao na haki zao. Watu wengi  hawawezi kurudi makwao. Wote sawia: Wakristo na Waislamu, wanayapita mateso haya makubwa kama matokeo ya wachache wanaodai kuwa watu wa dini zaidi, ambao hulitumia jina la dini vibaya kwa kutengeneza itikadi zao za kidini kwa  maslahi yao kupitia dhuluma na vifo.

Katika hali hizo, Papa anapenda kuwahakikishia kwamba yu karibu na Maaskofu na  wale wote wanaoishi mateso na unyanyasaji huo. Na kwamba kila siku anawakumbuka katika sala zake nakwa mara nyingie anapenda kuwatia shime na faraja kwa  maneno  ya kufariji ya Yesu Kristo, yanayopaswa kusikika daima ndani ya moyo wa kila mmoja: "Nawaachieni amani, amani yangu nawapa" (Yoh 14:27).

Amani, Papa ameendelea kusema, si tu kutokuwa na vita au kama  matokeo ya kukosekana kwa maelewano katika baadhi ya vipengere vya kisiasa, au ukosefu wa ubabe wa kupindukia. Lakini  Amani, ni  kwa ajili yetu, ni zawadi inayotoka kwa  Yesu Kristo mwenyewe, Mfalme wa amani, anayewafanya wawili kuwa sawa na mtu mmoja( Efe. 2:14). Na ni  tu wale wenye kupokea  amani ya Kristo ndani ya  mioyo  yao na kuihifadhi, kama mwanga wa kuwaongoza katika njia ya maisha  wanaweza kuwa  wajenzi wa amani (Rej. Mt 5,9.).

Wakati huo huo, amani ni utendaji wa  kila siku, wa kijasiri na halisi ya kukuza maridhiano na ushirikiano katika uzoefu wa maisha, kupanua ujenzi wa madaraja ya majadiliano, huduma kwa wanaoishi mazingira magumu na wanyonge zaidi waliotengwa.  Kwa neno moja, amani ni ujenzi wa utamaduni wa watu kukutana.

Katika Barua hii, Papa pia anapenda kutoa shukrani zake za  dhati  kwa Maaskofu,  kwa sababu  katikati ya majaribu mengi na mateso, Kanisa nchini  Nigeria, limeendelea kuhudumia kwa  ukarimu, huruma na msamaha. Na hivyo, amewakumbuka Mapadre, watawa na makatekista ambao licha ya kuhatarisha maisha yao, hawatelekezi kundi lao, bali wanaendelea kubaki  imara katika utumishi wao, huku wakihubiri na kuendelea kuwa waamini kwa Injili ya Kristo.

Kwao wote, Papa ametoa shukrani zake za dhati na kuonyesha mshikamano wake, na kuwataka wasichoke kutenda mema.  Kwa ajili yao alitolea shukurani ka Bwana pia kwa watu wengi toka pande mbalimbali za kijamii, kiutamaduni na kidini ambao kwa mapenzi yao na maamuzi yao thabiti, wamesimama imara kupinga kila aina ya ghasia na fujo, na kwa wale wote wenye  kupendelea neema ya usalama na utulivu  kwa ajili ya wote. 

Watu hao wanakuwa ni mfano mzuri unaotutia nguvu mpya  ya  kusonga mbele katika kushuhudia manufaa ya amani kama Papa Mstaafu  Benedikto wa XVI, alivyokumbusha  mwishoni mwa Sinodi kwa ajili ya  Afrika, Ni nguvu ya  Roho Mtakatifu ambayo hubadilisha mioyo ya waathirika na watesaji wao na hivyo kuweza kurejesha udugu" Dhamana ya Afrika, (Africae Munus, 20) .

 

Kwa maono haya Papa Francisko amewahimiza  ndugu zake Maaskofu wa Nigeria, kudumu katika uvumilivu na bila kukata tamaa, bali kusonga mbele  pamoja katika njia ya amani (Rej Lk 1:79.) na katika kuwaongoza  waathirika, kuwasaidia maskini na kuelimisha vijana ili wote waweze kuwa ni vyombo vya haki, amani na mshikamano wa kitaifa.

Mwishoni, Papa Francisko kupitia barua hii amewapatia baraka zake za Kitume, akiwataka pia wazifikishe kwa Familia ya Mungu nchini Nigeria pamoja na wote wanaoteseka kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Ufufuo wa Yesu kristo   uwe kichocheo cha: toba, wongofu, maridhiano na amani kwa watu wote wa Nigeria! Na mwisho kabisa amewakabidhi wananchi wote wa Nigeria chini ya ulinzi na maombezi ya Bikira Maria, Malkia wa Afrika. Na amewaomba kumkumbuka pia katika sala na sadaka yao.








All the contents on this site are copyrighted ©.