2015-03-02 08:40:00

Ushiriki mkamilifu katika Mafumbo ya Kanisa!


Mwenyeheri Paulo VI kunako tarehe 7 Machi 1967 kwa mara ya kwanza aliadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu kwa lugha ya Kiitalia, kwenye Parokia ya Watakatifu wote, Jimbo kuu la Roma, kama sehemu ya mchakato wa utekekelezaji wa mabadiliko makubwa yaliyofanywa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, ili Mwenyezi Mungu aweze kuabudiwa kikamilifu na mwanadamu kutakatifuzwa katika maisha yake.

Huu ukawa ni mwanzo wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu katika lugha mbali mbali, kikiwemo Kiswahili ili kuwawezesha waamini kushiriki kikamilifu katika Mafumbo ya Kanisa. Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linamwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani, kwani leo hii kuna ushiriki mkubwa wa waamini katika maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa, ikilinganishwa na wakati ule, Ibada ya Misa Takatifu ilipokuwa ikiadhimishwa kwa lugha ya Kilatini.

Huu ni utambuzi wa shughuli za kichungaji ulioliwezesha Kanisa kuona umuhimu wa kuisaidia Familia ya Mungu kufahamu na hatimaye, kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa, mchango mkubwa wa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika Liturujia ya Kanisa. Hivi ndivyo anavyofafanua Padre Giuseppe Midili, Mkurugenzi wa Idara ya Liturujia, Jimbo kuu la Roma, wakati huu, Mama Kanisa anapofanya kumbu kumbu ya miaka 50 tangu Familia ya Mungu nchini Italia na hatimaye, sehemu mbali mbali za dunia, ilipoanza maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kwa lugha ya Kiitalia.

Hii ni changamoto inayomtaka mwamini kutambua kwamba, adhimisho la Liturujia ni mchakato wa majadiliano ya kina kati ya Mwenyezi Mungu na mja wake, jambo lililosisitiziwa na Mwenyeheri Paulo VI. Waamini wanapaswa kusali na kuzungumza na Mwenyezi Mungu katika lugha wanayoifahamu, huu ukawa ni mwanzo pia wa utamadunisho wa Injili ya Kristo katika tamaduni mbali mbali duniani. Ushiriki mkamilifu wa waamini katika maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa unapata chimbuko lake msingi katika Sakramenti ya Ubatizo na kigezo muhimu katika mageuzi yaliyoletwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Baada ya changamoto hii, Mabaraza ya Maaskofu Katoliki sehemu mbali mbali yalianza kuunda kamati za kuangalia uwezekano wa kutekeleza taalimungu iliyokuwa imefafanuliwa na Mwenyeheri Paulo VI, ili iweze kutekelezwa katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa. Kanuni za mabadiliko ambazo zilipaswa kuzingatiwa katika kuandika vitabu vya Liturujia, zilibainishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika Waraka wake kuhusu Mabadiliko ya Liturujia, yaani “Sacrosanctum concilium”.

Hadi leo hii, Kanisa bado linaendelea kutekeleza changamoto za mabadiliko katika Liturujia zilizoletwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ndiyo maana hivi karibuni kumekuwepo na tafsiri mpya ya vitabu vya Liturujia, katika lugha ya Kiingereza na Kiswahili ili kuwawezesha waamini kukutana na kuzungumza na Kristo pamoja na kuhakikisha kwamba, waamini wanafanikiwa kumpeleka Kristo kwa Watu wa Mataifa kadiri ya lugha na tamaduni zao. Lengo ni kumwilisha imani katika wongofu wa ndani; kwa kutumia lugha na alama ambazo zinaeleweka vyema zaidi na Familia ya Mungu katika taifa husika.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume, Injili ya Furaha anabainisha kwamba, Kanisa linainjilisha na kuinjilishwa kwa njia ya ubora wa lugha inayotumiwa, ili kuwawezesha waamini kwa njia ya maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, kutambua chemchemi ya maisha ya Kikristo pamoja na kushiriki kikamilifu katika adhimisho la Fumbo la Pasaka. Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa na kamwe wasiwe ni wasikilizaji au watazamaji tu wa kile kinachoadhimishwa na Padre Altareni.

Lugha ya Kilatini bado inaendelea kutumiwa na Mama Kanisa kama lugha ya Kanisa, ndiyo maana katika maisha na utume wake, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliwahamasisha waamini kujifunza na kuipenda lugha ya Kilatini, kwani ni muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.