Serikali ya Tanzania imeyapokea maombi ya kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC)
cha Mkoa wa Mbeya yanayopendekeza mkoa huo ugawanywe na kupata mikoa miwili ya Mbeya
na Songwe. Akizungumza na maelfu ya wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika
Jumamosi, Februari 28, 2015, kwenye uwanja wa Saba Saba wilayani Chunya, Waziri Mkuu
Mizengo Pinda alisema Serikali imeridhia maombi hayo kutokana na ukubwa wa mkoa huo
ambao una kilometa za mraba 63,000.
“Tumekwishapokea maombi ya kuugawanya mkoa
wa Mbeya kwa sababu mkoa huu una eneo la kilometa za mraba 63,617 zilizogawanyika
katika Wilaya 8 na Halmashauri 10. Hili ni eneo kubwa sana kiutawala, siyo rahisi
kuusimamia na kusukuma maendeleo,” alisema.
Alisema kamati hiyo imeshauri mkoa
huo ugawanywe katika wilaya nne nne ambapo mkoa mpya wa Songwe utakuwa na wilaya za
Ileje, Momba, Mbozi na Chunya. Wamekubaliana kuwa makao makuu yatakuwa Mbozi lakini
ninyi wa chunya mmeenda mbali zaidi kwa kuigawa Chunya kwenye wilaya mbili za Songwe
na Chunya ambapo chunya itaenda Mbeya,” alisema Waziri Mkuu huku akishangiliwa.
Alisema
katika kikao hicho ilikubaliwa kwamba makao makuu ya wilaya mpya ya Songwe yatakuwa
Mkwajuni. “Nimekubali maombi haya kwa sababu yatapunguza gharama za uendeshaji, na
kama itashindikana kupata wilaya mpya basi itabidi tuwape Halmashauri ya Songwe,”
alisema. Mkoa wa Mbeya una wilaya nane ambazo zimegawanyika katika tarafa 27, kata
262, vijiji 842 na mitaa 252. Idadi ya wakazi kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi
ya mwaka 2012 ni 2,707,410.
Akizungumzia kuhusu mpango wa maji katika wilaya
hiyo, Waziri Mkuu alisema bado kuna changamoto kubwa ya kufikisha maji vijijini ambako
upatikanaji wake uko kwenye asilimia 46. “Tuna mpango wa kuchimba visima vikubwa vitatu
na mwakani tuna mpango wa kuchimba visima vingine virefu 11, tunachohitaji ni fedha
na usimamizi,” alisema.
Alivitaja vijiji viyakavyopata visima hivyo ni Makongorosi,
Mkwajuni, Kapalala, Isangawana, Galula, Lupa na Matwiga. Vingine ni Kambikatoto, Tanile,
Bitimanyanga na Mapogoro.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amezindua maabara tatu
katika shule ya sekondari ya Saza ambazo zimejengwa kwa ufadhili wa kampuni ya uchimbaji
dhahabu ya Shanta. Akitoa taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya
ya Chunya, Bi. Sophia Kumbuli alisema ujenzi wa maabara hizo tatu umegharimu sh. Milioni
268.5 vikijumuisha pia ununuzi wa samani, uwekaji wa mfumo wa maji na gesi.
“Kati
ya hizo sh. Milioni 23.5 ni za ununuzi wa vifaa vya maabara na kemikali na sh. Milioni
245 ni ujenzi wa jengo, samani na uwekaji wa mfumo wa maji na gesi,” alisema.
WAZIRI
MKUU AWAJULIA HALI MAJERUHI WA AJALI MBEYA
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda
amewatembelea askari wa Jeshi la Polisi waliolazwa kwenye Hospitali ya Mkoa wa Mbeya
kutokana na ajali waliyoipata Jumamosi wakati msafara wake ukielekea Kata ya Galula
wilayani Chunya. Waziri Mkuu aliwatembelea majeruhi hao na kuwapa pole Jumapili,
Machi Mosi, 2015) kabla ya kuelekea wilayani Mbozi kuendelea na ziara yake ya Mkoa
wa Mbeya. Alifuatana na mkewe Mama Tunu Pinda, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw. Abbas Kandoro
na Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Seif Mhina.
Akizungumzia hali ya majeruhi
hao, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dk. Ismail Macha alisema, Jumamosi walipokea
majeruhi tisa lakini watatu walifanyiwa uchunguzi wa afya zao na kuruhusiwa na wengine
sita ilibidi wawalaze na kuwafanyia uchunguzi zaidi kutokana na hali zao zilivyokuwa.
“Wengi wao walipata zaidi mshtuko ndiyo maana tukaamua kuwalaza ili tuendelee kuwapa
uangalizi wa karibu… Mmoja tu ndiye amevunjika mkono wa kulia lakini wengine walipata
michubuko miguuni, mikononi na usoni,” alisema.
Aliwataja waliolazwa kuwa ni
Deogratius Nandi (31), Paulin Masolwa (27), Omary Hussein (24), Hamisi Haji (29) ambao
wote ni wanaume. Majeruhi wa kike ni Cecilia Mussa Kabona (28) na Mwazanije Hassan
(23) ambaye amevunjika mkono wa kulia. Waliopata matibabu na kuruhusiwa ni Mashaka
Shabani (42), Khalifa Rashid (26) na Joel Cheja (21).
Kamanda wa Polisi Mkoa
wa Mbeya, Ahmed Msangi alisema chanzo cha ajali hiyo ni vumbi na kokoto barabarani
ambazo zilifanya gari hilo la FFU lisesereke na kupinduka. Hata hivyo, alisema mwendo
mdogo wa gari hilo ulisaidia kuokoa maisha ya askari hao.
“Ajali ilitokea saa
5:30 asubuhi eneo la Chang’ombe ya Mjele. Eneo lile lina kokoto kubwa kubwa ambazo
zilisababisha gari lao kuserereka na kupinduka… gari halikuwa kwenye mwendo mkali
ndiyo maana askari hao wamepata majeraha madogo madogo,” alisema.
UTORO
NA MIMBA ZA WANAFUNZI ZAMTIA KINYAA WAZIRI MKUU
Wakati huo huo Waziri
Mkuu Mizengo Pinda ameendelea kukemea tabia za utoro na mimba kwa wanafunzi wa shule
za msingi na sekondari wilayani Chunya baada ya kupewa taarifa kwamba watoto 4,420
walitoroka shule na wengine 201 kupata mimba. Februari 26, mwaka huu, Waziri Mkuu
aliwaagiza Mkuu wa Wilaya ya Kyela pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo
kuwasaka na kuwakamata wale wote waliohusika na utoro na ujauzito wanafunzi na kuwafikisha
mahakamani mara moja ili liwe fundisho kwa wengine baada ya kuelezwa kwamba wanafunzi
94 walipata ujauzito na wengine 645 kuacha shule kwa sababu ya utoro.
Akizungumza
na maelfu ya wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Jumamosi, Februari 28,
2015 kwenye uwanja wa Saba Saba wilayani Chunya, Waziri Mkuu alisema haiwezekani kuiacha
hali hiyo iendelee huku watoto wa wilaya hiyo wakiharibiwa maisha kwa kukosa masomo.
“Utoro kwenye shule za msingi, taarifa ya wilaya inaonyesha watoto 1,979 waliacha
shule kati ya mwaka 2010 na 2014 ambao ni wastani wa watoto 395 kila mwaka na katika
suala la mimba, taarifa hiyo inasema watoto 161 waliachishwa shule kwa sababu ya ujauzito,”
alisema.
“Haiwezekani kabisa! Hivi akinababa kuamua kutembea na mtoto shule
ya msingi ni lipi hasa unalolitaka kwake… unamwachisha shule mtoto kwa lipi hasa,
hapana. Nimeshatoa agizo wahusika wakamatwe. Wa zamani tunaweza tusiwapate, lakini
hawa wa mwaka jana kwa shule za msingi wako 28, RC na watendaji wako fuatilieni na
muwapeleke kwenye vyombo vya sheria,” alisisitiza. Akichanganua takwimu za sekondari,
Waziri Mkuu alisema kati ya mwaka 2010 na 2014 wanafunzi 2,251 waliacha shule kwa
sababu ya utoro na wengine 40 waliachishwa kwa sababu ya ujauzito.
“Ninawasishi
wazazi na uongozi wa wilaya na mkoa tufanye jitihada kuhakikisha jambo hili linakomeshwa
mara moja. Huwezi kununua madaftari an kumlipia ada tu halafu usitake kuona mwanao
anamaliza shule. Kila mzazi ana jukumu la kuhakikisha mtoto wake anamaliza shule ili
awe na maisha bora hapo baadaye,” alisema Waziri Mkuu. “Nirudie kuwakumbusha wazazi
kwamba mtoto wa mwenzio ni mtoto wako, huwezi kukubali maisha yaharibike hivi hivi.
Tuungane pamoja kuhakikisha tunashinda vita hii,”alisisitiza.