2015-03-02 09:27:52

Mchakato wa Katiba!


Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema kuna baadhi ya watu wamegeuza mchakato wa upatikanaji wa Katiba Mpya kuwa wa kisiasa badala ya kujikita kuwafahamisha wananchi mazuri yaliyomo. Ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akiwahutubia wakazi wa Kata ya Lwangwa kwenye Halmashauri ya Busokelo wilayani Rungwe akiwa kwenye siku ya nne ya ziara yake mkoani Mbeya kukagua shughuli za maendeleo.
“Katiba inayopendekezwa imezingatia maslahi ya kila kundi kwenye jamii hivyo zipuuzeni kauli zinazotolewa na baadhi ya watu kuwa Katiba hiyo haijakidhi malengo ya Kitaifa,”alisema. Alisema mabadiliko yaliyofanywa kwenye Katiba hiyo ni asilimia 20, huku asilimia iliyobakia ni sehemu ya mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Jaji Warioba. Alisema ili kukabiliana na kauli za kiupotoshaji, Serikali imeanza kusambaza nakala za Katiba inayopendekezwa hasa kwenye mikoa ya pembezoni.
“Jumla ya nakala 300 za Katiba Inayopendekezwa zitasambazwa kwenye kila Kata ambapo makundi yenye uwezo wa kutoa elimu sahihi kuhusiana na Katiba inayopendekezwa yatapatiwa nakala hizo ili kuwaelimisha wananchi,” alisema Waziri Mkuu.
Wakati huohuo, akiwa Tukuyu mjini, Waziri Mkuu alizindua ofisi za Halmashauri hiyo baada ya jengo la zamani kupata nyufa kutokana na tetemeko la ardhi. Pia alizindua maabara tatu kwenye shule ya sekondari ya wasichana ya Kayuki.
Akingumza na maelfu ya wakazi waliojitokeza kumsikiliza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa michezo wa Tandale jana jioni, Waziri Mkuu aliwataka wakazi hao kujitokeza kwa wingi na kujiandikisha wakazi zoezi la uboreshaji Daftari la Kudumu la Wapiga Kura litakapoanza.
Alisema ni muhimu wananchi watumie fursa hiyo ya kujiandikisha kwa sababu kadi zinazotolewa ndiyo zitatumika kwenye upigaji kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa pamoja na Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu.
“Usipojiandikisha sasa hutaweza kupiga kura kumchagua kiongozi unayemtaka wakati huo ukifika. Hata ukiwa na kitambulisho au barua gani hutaruhusiwa kwa sababu taarifa zako zitakuwa hazimo kwenye daftari la wapigakura.”
“Hili zoezi limeanza sasa pale Njombe na litafanyika nchini kote, ni vema tukijitokeza kwa wingi na kujiandikisha wakati waandikishaji watakapokuja hapa Tukuyu,” alisema Waziri Mkuu.
Katika hatua nyingine, Mbunge wa Rungwe Magharibi, Prof. Mwakyusa aliiomba Serikali iingilie kati mradi wa maji wa masoko kutokana na mradi huo kukwama kwa muda mrefu. “Mradi huu umelenga kuwanufaisha wanachi wa vijiji 15, mkataba ulisainiwa tangu 2009 na mradi ulipaswa kukamilika mwaka 2011 lakini hadi leo hakuna hata tone la maji,” alisema Prof. Mwakyusa.
Aliiomba Serikali pia iingalie barabara ya kutoka Tukuyu hadi Busokelo yenye urefu wa km. 86 kwani ni mkombozi wa mazao mengi yanayozalishwa kwenye Halmashauri ya Busokelo. “Hii barabara ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami na imeingizwa kwenye Ilani ya Uchaguzi. Kwa vile muda uliobakia ni mfupi, tunaomba iwekewe japo jiwe la msingi ili Rais ajaye akumbuke kuikamilisha,” alisema.








All the contents on this site are copyrighted ©.