Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema kuna baadhi ya watu wamegeuza mchakato
wa upatikanaji wa Katiba Mpya kuwa wa kisiasa badala ya kujikita kuwafahamisha wananchi
mazuri yaliyomo. Ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akiwahutubia wakazi wa
Kata ya Lwangwa kwenye Halmashauri ya Busokelo wilayani Rungwe akiwa kwenye siku ya
nne ya ziara yake mkoani Mbeya kukagua shughuli za maendeleo. “Katiba inayopendekezwa
imezingatia maslahi ya kila kundi kwenye jamii hivyo zipuuzeni kauli zinazotolewa
na baadhi ya watu kuwa Katiba hiyo haijakidhi malengo ya Kitaifa,”alisema. Alisema
mabadiliko yaliyofanywa kwenye Katiba hiyo ni asilimia 20, huku asilimia iliyobakia
ni sehemu ya mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Jaji Warioba. Alisema ili kukabiliana
na kauli za kiupotoshaji, Serikali imeanza kusambaza nakala za Katiba inayopendekezwa
hasa kwenye mikoa ya pembezoni. “Jumla ya nakala 300 za Katiba Inayopendekezwa
zitasambazwa kwenye kila Kata ambapo makundi yenye uwezo wa kutoa elimu sahihi kuhusiana
na Katiba inayopendekezwa yatapatiwa nakala hizo ili kuwaelimisha wananchi,” alisema
Waziri Mkuu. Wakati huohuo, akiwa Tukuyu mjini, Waziri Mkuu alizindua ofisi za
Halmashauri hiyo baada ya jengo la zamani kupata nyufa kutokana na tetemeko la ardhi.
Pia alizindua maabara tatu kwenye shule ya sekondari ya wasichana ya Kayuki. Akingumza
na maelfu ya wakazi waliojitokeza kumsikiliza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika
kwenye uwanja wa michezo wa Tandale jana jioni, Waziri Mkuu aliwataka wakazi hao kujitokeza
kwa wingi na kujiandikisha wakazi zoezi la uboreshaji Daftari la Kudumu la Wapiga
Kura litakapoanza. Alisema ni muhimu wananchi watumie fursa hiyo ya kujiandikisha
kwa sababu kadi zinazotolewa ndiyo zitatumika kwenye upigaji kura ya maoni ya Katiba
Inayopendekezwa pamoja na Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu. “Usipojiandikisha
sasa hutaweza kupiga kura kumchagua kiongozi unayemtaka wakati huo ukifika. Hata ukiwa
na kitambulisho au barua gani hutaruhusiwa kwa sababu taarifa zako zitakuwa hazimo
kwenye daftari la wapigakura.” “Hili zoezi limeanza sasa pale Njombe na litafanyika
nchini kote, ni vema tukijitokeza kwa wingi na kujiandikisha wakati waandikishaji
watakapokuja hapa Tukuyu,” alisema Waziri Mkuu. Katika hatua nyingine, Mbunge
wa Rungwe Magharibi, Prof. Mwakyusa aliiomba Serikali iingilie kati mradi wa maji
wa masoko kutokana na mradi huo kukwama kwa muda mrefu. “Mradi huu umelenga kuwanufaisha
wanachi wa vijiji 15, mkataba ulisainiwa tangu 2009 na mradi ulipaswa kukamilika mwaka
2011 lakini hadi leo hakuna hata tone la maji,” alisema Prof. Mwakyusa. Aliiomba
Serikali pia iingalie barabara ya kutoka Tukuyu hadi Busokelo yenye urefu wa km. 86
kwani ni mkombozi wa mazao mengi yanayozalishwa kwenye Halmashauri ya Busokelo. “Hii
barabara ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami na imeingizwa
kwenye Ilani ya Uchaguzi. Kwa vile muda uliobakia ni mfupi, tunaomba iwekewe japo
jiwe la msingi ili Rais ajaye akumbuke kuikamilisha,” alisema.