CERNA, wahudumu wa matumaini Kaskazini mwa Afrika!
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kaskazini mwa Afrika, CERNA, limehitimisha
hija yake ya kitume inayofanyika walau kila baada ya miaka mitano mjini Vatican kwa
kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu pamoja na viongozi waandamizi kutoka Vatican.
Maaskofu hawa wamemkabidhi Baba Mtakatifu nakala ya barua ya kichungaji kwa ajili
ya Familia ya Mungu Kaskazini mwa Mwafrika inayoongozwa na kauli mbiu “Watumishi wa
matumaini, Kanisa Katoliki Kaskazini mwa Afrika kwa nyakati hizi”.
Barua hii
imegawanyika katika ibara kuu nne zinazogusia: Mageuzi Kaskazini mwa Afrika; maendeleo
ya Makanisa mahalia; utume na ushuhuda wa Makanisa haya; ufuasi kwa Bikira Maria.
Maaskofu
wanabainisha kwamba, cheche za mapinduzi ya Nchi za Kiarabu, athari za myumbo wa uchumi
kimataifa na ongezeko kubwa la wimbi la wahamiaji kutoka ndani na nje ya Bara la Afrika
ni kati ya changamoto kubwa ambazo Kanisa linakabiliana nazo huko Kaskazini mwa Afrika,
kiasi hata cha kutishia mchakato wa ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika matendo.
Hii ni changamoto kubwa katika uhuru wa kuabudu na kwamba, mambo yote haya
yanaathari kubwa katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Afrika ya Kaskazini. Uhuru
wa kuabudu, utu na heshima ya binadamu, maridhiano ndani ya jamii na tunu msingi za
kimaadili ni mambo msingi katika mfungamano wa kijamii. Maaskofu wanataka wakuu wa
nchi Kaskazini mwa Afrika kuhakikisha kwamba, wanaendeleza na kudumisha misingi hii
kama kipimo cha ubora wa mchakato wa demokrasia ya kweli.
Sera na mikakati
ya kudhibiti wimbi kubwa la wahamiaji na wakimbizi, hazina budi kuhakikisha kwamba,
zinalinda na kuheshimu utu wa binadamu na haki zake msingi. Wananchi wote wahudumiwe
pasi na ubaguzi wa kidini, kwani kwa siku za hivi karibuni kuomenekana dalili za Wakristo
kutengwa katika huduma kwa wakimbizi na wahamiaji, jambo ambalo si haki kabisa. Ikumbukwe
kwamba, Kanisa limekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji,
kumbe, wanapaswa kutambuliwa na kuthaminiwa na jamii na kwamba, uhuru wa kidini hauna
budi kuheshimiwa ili kutoa nafasi kwa Wakristo pia kushiriki katika ibada mbali mbali,
lengo ni kushiriki katika mchakato unaopania kuwajengea matumaini kwa leo na kesho
iliyo bora zaidi.
Maaskofu Kaskazini mwa Afrika wanabainisha kwamba, majadiliano
ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam ni kati ya vipaumbele vyao vya mikakati na
shughuli za kichungaji. Kanisa linapenda kujenga madaraja ya watu kukutana na kusaidiana
katika umoja, upendo na udugu kwa kutambua kwamba, tofauti zao za kiimani ni utajiri
mkubwa unaopaswa kumwilishwa katika uhalisia wa maisha. Haya ni majadiliano yanayojikita
katika maisha ya watu. Wananchi wawe huru kufuata dhamiri zao nyofu, kwa kulinda na
kudumisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni, bila kupoteza utambulisho
wao wa kidini.
Maaskofu wanaendelea kubainisha kwamba, wanapenda kujikita
katika majadiliano ya kiekumene, ili Wakristo wakiwa wameshikamana na kushibana, waweze
kutolea ushuhuda kwa tunu msingi za maisha ya Kikristo katika sala inayomwilishwa
kwenye misingi ya haki, amani na upatanisho. Jumuiya za Kikristo Kaskazini mwa Afrika
hazina budi kuwa ni maabara ya kiekumene; mahali pa kuwafunda vijana tunu msingi za
maisha ya Kiinjili; imani, maadili na utu wema; ili kuweza kumshuhudia Kristo na Kanisa
lake kati ya mataifa. Kanisa litaendelea kutoa majiundo ya awali na endelevu ili kuwasaidia
vijana kusoma alama za nyakati, tayari kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao.
Maaskofu
wanapembua kwa kina na mapana shughuli mbali mbali zinazofanywa na Kanisa katika huduma
kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, kwani hawa kimsingi wanaionesha
ile sura ya Kristo. Kanisa pia halina budi kupewa haki zake msingi na kwamba ni sehemu
ya Familia ya Mungu, Kaskazini mwa Afrika na wala si kilaka kama ambavyo baadhi ya
watu wanadhani. Kanisa linapenda kuchangia katika mchakato wa ustawi na maendeleo
ya watu Kaskazini mwa Afrika.
Maaskofu wanasema kwamba, ndoa mseto ni kati
ya changamoto nyingine kubwa inayowakabili katika utekelezaji wa shughuli zao za kichungaji.
Licha ya tofauti za kiimani na kitamaduni, ikiwa kama wanandoa wataheshimiana na kuthaminiana,
ndoa yao inaweza kuwa ni baraka kubwa ndani ya jamii. Kumbe kuna haja ya kudumisha
uhuru wa dhamiri, majadiliano ya kidini, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa utu na
heshima ya binadamu. Sera hizi zijioneshe pia katika masuala ya uchumi na maendeleo
ya watu. Kanisa linapenda kuchangia katika mchakato wa maendeleo endelevu: kiroho
na kimwili.
Mwishoni, Maaskofu wanawaalika waamini kujifunza kutoka kwa Bikira
Maria, Mama aliyeyakita maisha yake katika sala na kwamba, kilele cha maisha ya kiroho
kijioneshe kwa waamini kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi
Takatifu. Waamini wajitahidi kujenga mahusiano mema na jirani zao kama njia ya ushuhuda
wa maisha ya imani yanayomwilishwa katika matendo. Waoneshe upendo na ukarimu kwa
majirani na maskini kwani Kanisa linapenda kuwakutanisha watu katika hija ya maisha
yao ya kiroho, ili kuwajengea na kuwaimarisha katika imani na matumaini kwa Mwenyezi
Mungu.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican.