2015-02-28 07:50:50

Wosia wangu kwenu: Sala na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu


Jumuiya ya wanafunzi Wakatoliki pamoja na watanzania wanaoishi na kufanya shughuli zao mjini Roma, tarehe 26 Februari 2015 waliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu mteule Liberatus Sangu wa Jimbo Katoliki Shinyanga, ili kumshukuru Mungu kwa matendo yake makuu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Jimbo Katoliki la Shinyanga kwa kumpata Mchungaji mkuu. Ibada hii imefanyika kwenye Kikanisa cha Chuo cha Mtakatifu Paulo, mjini Roma. RealAudioMP3

Katika mahubiri yake, Askofu mteule Sangu, amewataka Mapadre na Watawa kwa namna ya pekee kabisa kujenga na kudumisha Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu kwani hapa ni mwanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa. Anatambua kwamba, wanashiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, lakini Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu inawasaidia kupyaisha maisha, utume na dhamana ambayo wamekabidhiwa na Mama Kanisa katika maisha yao.

Muda wa saa moja, unatosha kabisa kukaa mbele ya Ekaristi Takatifu ili kuzungumza na Kristo pamoja na kumwachia nafasi ya kukushirikisha mapenzi yake katika maisha na utume wako. Kwa njia ya Ibada ya kuabudu Ekaristi Takatifu, watafanikiwa kuwagusa na kuwasaidia watu katika hija ya maisha yao ya kiroho na kimwili. Mapadre na Watawa wajifunze kutoka kwa Mtakatifu Yohane Paulo II pamoja na watakatifu wengine wa Kanisa waliotumia muda wao mwingi kuabudu Ekaristi Takatifu.

Huu ndio wosia na zawadi kubwa ambayo Askofu mteule Libertaus Sangu amependa kuiachia Jumuiya ya Watanzania wanaoishi na kusoma mjini Roma, wakati huu anapoanza ukurasa mpya wa maisha yake kama Mchungaji mkuu wa Jimbo Katoliki la Shinyanga.

Askofu mteule Sangu anasema kwamba, Mwenyezi Mungu daima anasikiliza sala za waja wake na kuzijibu kwa wakati muafaka. Kuteuliwa kwake na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Shinyanga ni matokeo ya sala na sadaka ya Familia ya Mungu Jimboni Shinyanga, iliyosali na kumlilia Mwenyezi Mungu ili awapatie Mchungaji mkuu baada ya kufariki kwa Askofu Aloysius Balina, zaidi ya miaka miwili iliyopita. Mwenyezi Mungu anasikiliza sauti ya waja wake hata katika udhaifu wao na atawajibu kwa wakati wake.

Askofu mteule Sangu anasema kwamba, waamini hawana budi kumwilisha sala katika maisha na vipaumbele vyao sanjari na kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao, jambo ambalo wakati mwingine si rahisi sana. Anasema, amekubali kuwa Askofu wa Shinyanga kama sehemu ya utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro na katika kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yake na kwamba, anajiaminisha mikononi mwake Yeye aliyemteua kwa matumaini kwamba, atamwezesha kutekeleza wajibu wake wa kufundisha, kuongoza na kuwatakasa Watu wa Mungu kadiri ya mapenzi ya Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.